Makala

Utu wa polisi wadhihirika wakimsaidia mlemavu aliyekwama kwenye maandamano

Na BENSON MATHEKA May 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

UTU wa polisi ulijitokeza kwa namna ya kipekee wakati wa maandamano yaliyotikisa mji wa Machakos, Mei 18, 2026 pale maafisa wa usalama walipoonekana wakimsaidia mwanamume mlemavu aliyekuwa amenaswa katika vurugu akielekea hospitalini.

Tukio hilo lilishuhudiwa katikati ya taharuki iliyosababisha kufungwa kwa biashara, shule na kusimama kwa shughuli mbalimbali katika mji wa Machakos huku barabara ya Machakos–Kitui ikifungwa na waandamanaji.

Polisi walimwagwa maeneo mbalimbali kujaribu kurejesha utulivu na kuwashawishi vijana kufungua njia.

Hali ilianza kuwa tete asubuhi baada ya baadhi ya waendesha bodaboda na madereva wa magari binafsi kusitisha shughuli zao wakitaja mgomo uliotarajiwa kuanza saa nne asubuhi.

Hata hivyo, baadhi yao waliendelea kutoa huduma kwa wagonjwa na dharura, wakibeba majeruhi na waliohitaji matibabu.

Maafisa wa polisi wakimsaidia mwanamume mlemavu kuabiri bodaboda Machakos, Mei 18, 2026. Picha|Benson Matheka

 

Katika hali ya kushangaza, afisa mmoja wa polisi alionekana akimwendea mwanaume mlemavu aliyekuwa amekwama katikati ya vurugu hizo na kumsaidia kufika kwenye bodaboda.

Afisa huyo alimsaidia kupanda kwenye pikipiki hiyo na baadaye kulipia nauli yake ili aharakishe kufikishwa hospitalini.

Wakazi waliokuwa eneo hilo walieleza kuwa tukio hilo lilitoa taswira tofauti ya maafisa wa polisi, ikionyesha huruma na ubinadamu katikati ya mazingira magumu ya usalama.

Hata hivyo, hali katikati ya mji wa Machakos iliendelea kuwa ya wasiwasi baadaye mchana baada ya mapambano makali kati ya polisi na waandamanaji, ambapo gesi ya kutoa machozi na risasi za mpira zilirushwa kuwatawanya vijana waliokuwa wakiziba barabara.

Ilikuwa afueni kubwa kwa mwanamume huyo pale alipofaulu kukalia bodaboda vizuri tayari kwenda hospitalini wakati ambapo maandamano ya kulalamikia bei za mafuta yalikuwa yamepamba moto Machakos. Picha|Benson Matheka

 

Katika tukio jingine la kusikitisha, afisa wa polisi alikimbizwa hospitalini baada ya mkebe wa gesi ya kutoa machozi kulipuka mkononi mwake alipokuwa akijiandaa kuurusha kuelekea kwa waandamanaji.

Licha ya ghasia hizo, tukio la kumsaidia mlemavu limebaki kuwa alama ya utu katikati ya mvutano mkali uliotawala Machakos.