Habari

Gachagua alivyowabwaga Ruto, Kindiki kwenye uchauzi wa Ol-Kalou

Na MWANGI MUIRURI July 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

NAIBU Rais Kithure Kindiki alipomuahidi mtangulizi wake Rigathi Gachagua kichapo kikali katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou baada ya kifo cha Mbunge David Kiaraho, huenda hakutambua kuwa hangeweza kuipa serikali ushindi katika uchaguzi huo.

Matokeo yaliyotangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Julai 17, 2026 yalionyesha mgombeaji wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), Sammy Kamau Ngotho, alishinda kwa kura nyingi.

Bw Ngotho alipata kura 35,440, sawa na takriban asilimia 85 ya kura zilizopigwa, huku mgombea wa United Democratic Alliance (UDA), Muchina Nyaga, akipata kura 5,450 pekee.

Ushindi huo, kwa mujibu wa wachambuzi, ulianza miezi kadhaa kabla ya kampeni rasmi.

Akiwa Meru mwezi Aprili, Prof Kindiki alisema serikali ingemkabili Bw Gachagua na kumshinda kisiasa.

Lakini Bw Gachagua alijibu kwa kumkumbusha kuwa katika mila za Agikuyu, si vyema kuanza siasa kabla marehemu hajazikwa.

Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Kikuyu, Wachira Kiago, anasema kauli hiyo iligeuza mtazamo wa wananchi.

“Bw Gachagua alifanya serikali ionekane kana kwamba ilikuwa ikisherehekea kifo cha mbunge ili kupata nafasi ya uchaguzi. Marehemu huheshimiwa sana kulingana na mila zetu,” alisema.

Katika mazishi ya Mbunge David Kiaraho, Bw Gachagua aliibuka kuwa kivutio kikuu.

Alizungumza kwa muda mrefu kuliko Rais William Ruto, akawakosoa viongozi wa serikali na hata kuongoza kwaya iliyoburudisha waombolezaji.

Mchambuzi wa siasa Malila Munywoki anasema serikali ilipokuwa bado ikiomboleza, DCP tayari ilikuwa imeanza kampeni.

Anasema hatua nyingine muhimu ilikuwa pale Seneta wa Nyandarua John Methu alipomwambia Rais kuwa anamuheshimu kama Amri Jeshi Mkuu lakini hamwogopi.

“Hapo ndipo vita vya kisiasa vilipoanza rasmi,” alisema.

Bw Gachagua baadaye alimpongeza Bw Methu kwa mchango wake katika ushindi huo.

“Niliahidi kulea kizazi kipya cha viongozi. Nilimpa John Methu na Wanjiku Muhia jukumu la kuongoza kampeni ili kuona kama wamekomaa. Leo ninathibitisha kuwa John Methu amekomaa,” alisema.

Mwanasiasa huyo pia alimfanya Bw Methu kuwa Katibu Mkuu wa muda wa DCP.

Mchambuzi wa siasa John Okumu anasema hatua hiyo iliwafanya wananchi wa Nyandarua kuhisi kuwa walikuwa wakipigania mmoja wao.

“DCP ilionekana kuwa chama cha Nyandarua. Watu walihisi wakimpigania Methu walikuwa wakijipigania wenyewe,” alisema.

Baada ya hapo, Bw Gachagua alianza kueneza ujumbe kuwa Nyandarua ni kitovu cha mapambano ya uhuru na kwamba eneo la Mlima Kenya lilikuwa limetengwa na serikali iliyosaidia kuingia madarakani mwaka 2022.

Mchambuzi wa siasa Herman Manyora anasema ujumbe huo ulimgeuza Rais Ruto kuwa adui wa kisiasa wa eneo la Mlima Kenya.

“Aliwafanya wananchi waamini uchaguzi huo ulikuwa mapambano ya kujikomboa kutokana na usaliti,” alisema.

Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri anakiri kuwa serikali iliingia kwenye uchaguzi huo ikiwa katika nafasi ngumu.

“Ni kweli tulianza tukiwa na takriban asilimia tisa pekee ya uungwaji mkono. Kwa karibu miezi 20 Bw Gachagua alikuwa akiishambulia serikali kila siku. Tulikuwa nyuma tangu mwanzo,” alisema.

Hata hivyo, alisema serikali haikuwa na budi kusimamisha mgombeaji na kupambana hadi mwisho.

Kwa mujibu wake, kura zilizopatikana zinaonyesha UDA iliongeza uungwaji mkono kutoka asilimia tisa hadi asilimia 13.

Anaamini ndani ya mwaka mmoja uliosalia kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027, pengo hilo linaweza kupunguzwa zaidi.

Lakini Profesa Peter Kagwanja hakubaliani na tathmini hiyo.

Anasema matokeo ya Ol Kalou yanapaswa kuchukuliwa kwa uzito.

“Ni wakati wa kukubali ukweli. Inaonekana Mlima Kenya umebadilika kisiasa na hauonekani kutaka kurejea. Kama ningekuwa namshauri Rais Ruto, ningemwambia mkakati wake wa kuchaguliwa tena haupaswi kutegemea kura za Mlima Kenya pekee,” alisema.

Kampeni hizo pia zilitawaliwa na matumizi makubwa ya fedha.

Aliyekuwa mshauri wa kiuchumi Moses Kuria aliwahi kudai kuwa serikali ilikuwa imetenga zaidi ya Sh10 bilioni kugharimia miradi ya maendeleo na shughuli za kampeni.

Mbunge wa Nakuru Mashariki David Gikaria pia alisema wakati wa kampeni kuwa zaidi ya Sh1.2 milioni zilikuwa zikitumika kila siku katika kila wadi kwa shughuli za kuwafikia wapigakura.

Kwa upande wa DCP, chanzo kilicho karibu na timu ya kampeni kilidai Bw Gachagua alikuwa akitoa takriban Sh2 milioni kila siku.

Chanzo hicho kilisema zaidi ya Sh150 milioni zilitolewa na Bw Gachagua huku zaidi ya Sh180 milioni zikichangwa na mgombeaji wa DCP na wafuasi wengine.

Mbunge wa Kipipiri Wanjiku Muhia alisema mafanikio ya DCP yalitokana na ushirikiano mkubwa wa viongozi wa mashinani, hasa madiwani.

“Tulikuwa na ujumbe mmoja wa ukombozi. Tuliwaambia wananchi kwamba pesa na zawadi walizopewa zilikuwa mali yao wenyewe iliyokuwa inarudishwa kwao,” alisema.

Alisema chama hicho pia kilitumia kwa ufanisi redio za lugha za wenyeji na mitandao ya kijamii kufikisha ujumbe wake.

Kwa mujibu wa Seneta Methu, Bw Gachagua hakuonekana sana majukwaani lakini aliendelea kuongoza kampeni akiwa nyuma ya pazia.

Alikuwa akiwapigia simu wapigakura moja kwa moja wakati wa mikutano na kutoa mwelekeo wa ujumbe wa kampeni.

Bw Methu pia alisema hatua ya Bw Gachagua kuendelea kuikosoa IEBC na idara za usalama kuhusu madai ya matumizi ya wahuni ilisaidia kuweka uchaguzi huo chini ya uangalizi wa taifa.