Korti yaagiza meli ghali ya mihadarati iliyonaswa Mombasa iharibiwe
MELI ya Iran kwa jina MV Mashallah pamoja na dawa za kulevya aina ya methamphetamine zenye thamani ya Sh8.2 bilioni, zitaharibiwa kufuatia amri ya mahakama.
Mahakama ilitoa amri hiyo kutokana na hofu ya ukiukaji wa usalama, ufisadi, wizi na uwezekano wa magenge ya uhalifu kuvamia na kurejesha dawa hizo kwa umma.
Mahakama ya Shanzu iliamua kuwa kiasi hicho cha dawa pamoja na thamani yake kubwa ya kifedha zinaibua hofu kubwa kuhusu usalama ambayo haiwezi kupuuzwa.
Mahakama pia ilieleza wasiwasi kuhusu usalama wa maafisa waliokabidhiwa jukumu la kuhifadhi mzigo huo, ikisema wako katika hatari ya kushawishiwa kwa njia zinazoweza kuathiri uaminifu na hadhi yao ya kitaaluma.
Mahakama pia ilibaini kuwa, biashara ya dawa za kulevya kwa kiwango kilichoonyeshwa katika kesi hiyo inavuka mipaka ya sheria ya kawaida ya uhalifu na kugusa uhalifu wa kimataifa uliopangwa, usalama wa baharini na uthabiti wa kikanda.
Mahakama iliamuru mzigo huo uharibiwe ndani ya siku 30 kuanzia Mei 15. Dawa hizo zenye uzani wa kilo 1,036.044 zinahifadhiwa katika kambi ya Jeshi la Wanamaji nchini, eneo la Mtongwe, Mombasa.
Mahakama ilimwelekeza Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Mazingira (NEMA) kuamua njia ya kuharibu dawa hizo.
Dawa hizo pamoja na vifurushi vyake pia vitapimwa tena na kuharibiwa mbele ya mahakama, upande wa mashtaka, washukiwa, wakili wao na wawakilishi wa mashirika mbalimbali.
Mahakama pia iliamuru kuwa ni maafisa walioidhinishwa pekee watakaosimamia usafirishaji wa mzigo huo kutoka kituo cha Jeshi la Wanamaji hadi eneo la uharibifu.
Dawa hizo zitafungwa kwenye magari salama ya usafiri, kusindikizwa na maafisa wa usalama wenye silaha na hazitaachwa bila uangalizi hadi zitakapoharibiwa kikamilifu.
Zaidi ya hayo, uharibifu huo utafanywa kwa mujibu wa kanuni za uchunguzi na utupaji wa vitu vilivyonaswa, ikimaanisha kuwa kila kontena au kifurushi cha dawa kilichonaswa lazima kikaguliwe na orodha ya bidhaa kuandaliwa.
Dawa hizo pia zitathibitishwa na kulindwa ili kuhakikisha zinahesabiwa kikamilifu tangu ziondolewe kwenye hifadhi hadi wakati wa kuharibiwa kabisa.
“Baada ya uharibifu kutakuwa na cheti cha kuthibitisha kuwa zimeharibiwa kikamilifu. Magunia yahifadhiwe na yabaki chini ya uangalizi wa afisa mpelelezi ili yatolewe wakati wa kesi iwapo kutakuwa na haja,” mahakama iliamua.
Upimaji upya, usafirishaji, uharibifu, uhifadhi na utunzaji wa magunia pia vitarekodiwa kupitia vyeti, video na ushahidi wa picha.
Mahakama pia ilisema kuwa pingamizi dhidi ya uharibifu huo, ingawa iliegemezwa ipasavyo kwenye nia ya kupata kesi ya haki, haikuonyesha madhara yoyote mahsusi ambayo yangetokana na kuharibiwa kwao.
Hii si mara ya kwanza kwa Kenya kuharibu vyombo vya baharini na mizigo ya dawa zilizokamatwa baharini katika jitihada za kudhibiti biashara ya dawa za kulevya.
Agosti 14, 2015, Jeshi la Wanamaji la Kenya liliharibu boti ya kifahari iliyopatikana na kilo 7.5 za heroini zenye thamani ya Sh29 milioni katika eneo la Delta 16 kwenye kina kirefu cha Bahari ya Hindi.
Katika operesheni kama hiyo mwaka wa 2014, Kenya iliharibu heroini ya majimaji na ya unga yenye thamani ya Sh1.3 bilioni pamoja na meli iliyokamatwa bahari kuu.
Meli hiyo, MV Al Noor, iliharibiwa pamoja na mzigo wake kama sehemu ya juhudi za serikali kuonyesha dhamira ya kupambana na biashara ya dawa za kulevya.