Akili MaliMakala

Hasara ambayo wauzaji maua nje ya nchi walikadiria wakati wa mgomo wa matatu

Na SAMMY WAWERU May 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 4

BARAZA la Maua Kenya (KFC) linakadiria kuwa kati ya tani 100 hadi 200 za maua zilizokuwa zimepangwa kusafirishwa nje ya nchi mnamo Jumatatu, Mei 18, 2026, zilicheleweshwa au kuathirika kwa viwango tofauti kutokana na maandamano yaliyofanyika nchini dhidi ya bei ya mafuta ya petroli.

Maandamano hayo yaliyoitishwa na wamiliki wa matatu, wahudumu wa magari ya uchukuzi wa umma, madereva wa malori, wamiliki wa magari binafsi, pamoja na waendesha teksi, yalianza Jumatatu baada ya mazungumzo kati yao na serikali kuhusu bei ya mafuta kukosa kuafikiana.

Kulingana na KFC, baraza linaloleta pamoja wakulima na wauzaji wa maua, sekta hiyo ilikabiliwa na hasara ya moja kwa moja ya takriban Sh200 milioni siku ya Jumatatu pekee kutokana na kucheleweshwa kwa mizigo na uwezekano wa kuharibika kwa maua, bila kusahau bei ya soko la kimataifa na gharama za usafirishaji.

Katika taarifa, KFC ilieleza wasiwasi wake kuhusu kuongezeka kwa hasara huku maandamano hayo yakifanyika siku ya pili, Jumanne, Mei 19, ikisema kuwa yamevuruga kwa kiasi kikubwa usafirishaji wa wafanyakazi, mizigo na huduma muhimu za usafirishaji zinazopiga jeki sekta ya maua nchini.

“Sekta ya maua hutegemea sana mifumo ya usafirishaji inayohitaji kuzingatia muda, pamoja na usafirishaji wa mifumo baridi (cold chain systems) ili kupeleka maua mabichi kutoka mashambani hadi Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Jomo Kenyatta (JKIA) kwa ajili ya kusafirishwa katika masoko ya kimataifa. Misukosuko ya Jumatatu iliathiri wafanyakazi kufika shambani, kuchelewesha usafirishaji wa mizigo na kuvuruga shughuli zilizopangwa za usafirishaji wa nje,” alisema Afisa Mkuu Mtendaji wa KFC, Clement Tulezi.

Bw Tulezi alisema wafanyakazi wengi wa mashambani walikumbwa na ugumu kufika sehemu zao za kazi kwa sababu ya vizuizi barabarani, uhaba wa magari ya umma na kuzuiwa kwa shughuli katika barabara kuu.

Maafisa wa polisi wa kukabiliana na ghasia (GSU), kwa ushirikiano na wale wa kawaida na wa utawala (AP) walitumwa katika maeneo yaliyoathirika kutawanya waandamanaji waliokuwa wakitaka kupunguzwa kwa bei ya mafuta, huku barabara kuu zinazoelekea miji mbalimbali zikifungwa kwa vizuizi.

Mfanyakazi kwenye shamba la kampuni ya maua akiyavuna. Picha|Sammy Waweru

Maandamano hayo yalishuhudiwa katika miji mikuu, ikiwemo Nairobi, Thika, Nyeri, Meru, Nakuru, Eldoret, Kisii na Kakamega, huku biashara nyingi zikikadiria hasara kutokana na ucheleweshaji wa usafiri, vurugu na uporaji wa mali uliofanywa na wahalifu waliojiunga na maandamano hayo.

KFC ilisema kuwa katika maeneo yanayokuzwa maua, ucheleweshaji wa wafanyakazi kuingia kazini uliathiri ratiba za uvunaji, kufunga mashada ya maua, uratibu wa usafirishaji na maandalizi ya kuuza maua nje ya nchi.

“Sekta ya maua hufanya kazi kupitia mfumo wa kimataifa unaozingatia sana muda ambapo upesi na kutegemewa ni vigezo muhimu. Maua ni bidhaa zinazoharibika haraka zinazolengwa na masoko ya kimataifa ambayo yanaendelea kufanya kazi licha ya changamoto za ndani ya nchi,” ilisema KFC.

Bw Tulezi alionya kuwa ucheleweshaji wa mizigo unaongeza hatari ya maua kuharibika, hasara za kifedha, adhabu za kimikataba, kupungua kwa imani ya wanunuzi na kupoteza ushindani wa muda mrefu kwa wakulima wa Kenya katika soko la kimataifa.

Utafiti wa awali wa KFC ulionyesha kuwa mahudhurio katika mashamba kadhaa ya maua yalipungua kwa kati ya asilimia 3 hadi 10 kutokana na changamoto za usafiri. Malori yaliyokuwa yakisafirisha maua kuelekea JKIA, pia, yalicheleweshwa sana kwa sababu ya kufungwa kwa barabara na kuzuiwa kwa shughuli za usafiri na uchukuzi Nairobi.

KFC iliongeza kuwa ratiba za usafirishaji wa maua yanayoharibika haraka zimevurugwa, jambo linaloongeza hatari ya kushuka kwa ubora wa maua hayo na kukataliwa katika masoko ya nje.

Hali hiyo ilikumba sekta ya maua wakati ambapo tayari inakabiliana na gharama kubwa za usafirishaji wa kimataifa – kwa njia ya ndege, kupungua kwa nafasi za mizigo ya anga na mivutano ya kisiasa duniani inayovuruga mifumo ya usambazaji.

Wakati Kenya ikikumbwa na changamoto za usafirishaji wa ndani kwa ndani, wauzaji wa kimataifa na wateja bado wanatarajia kupokea bidhaa kwa wakati, ubora faafu na upatikanaji usiokatizwa.

Takwimu za hivi karibuni za sekta hiyo zinaonyesha kuwa sekta ya maua nchini tayari imekuwa ikipoteza hadi Dola 1.4 milioni (karibu Sh180 milioni) kila wiki kutokana na changamoto za mizigo na usafirishaji zinazohusishwa na migogoro ya kimataifa haswa vita kati ya Israili na Iran, kupanda kwa gharama za usafirishaji na kuyumba kwa mifumo ya usambazaji.

Maandamano yaliyofanyika mapema wiki hii yaliongeza ugumu kwa kuvuruga shughuli za usafirishaji wa ndani na mauzo ya mizigo nje ya nchi.

Mnamo Jumatatu na Jumanne, barabara kuu jijini Nairobi zilisalia kufungwa, shughuli za usafiri wa umma zikisimama huku usafiri kote nchini ukivurugika kwa kiasi kikubwa.

Shada la maua tayari kuingia sokoni. Picha|Sammy Waweru

Ingawa KFC ilikiri kuwepo kwa shinikizo la kimataifa la bei ya mafuta na nishati linaloathiri uchumi wa dunia, Bw Tulezi alisema hali hiyo inaonyesha haja ya dharura kwa Kenya kuimarisha ustahimilivu wa mifumo yake ya usafirishaji, ugavi na nishati ili kulinda sekta muhimu za mauzo ya nje dhidi ya misukosuko ya mara kwa mara.

“KFC inatoa wito wa kuchukuliwa kwa hatua za haraka na zilizoratibiwa ili kupunguza hasara zinazoandama wafanyabiashara na wafanyakazi kutokana na kuyumba kwa bei ya mafuta na changamoto za usafirishaji. Kipaumbele kinapaswa kuelekezwa katika kurejesha huduma za kawaida za usafiri, kusaidia sekta zinazotegemea mauzo ya nje dhidi ya kupanda kwa gharama za mafuta na usafirishaji, kuhakikisha mizigo inasafirishwa kwa urahisi na kuimarisha ustahimilivu wa muda mrefu kwa sekta muhimu za mauzo ya nje kama vile kilimo cha maua,” alisema.

Baraza hilo lilionya kuwa bila hatua za haraka, vurugu za usafirishaji, kupanda kwa bei ya mafuta na shinikizo la kimataifa la usafirishaji zinaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa mauzo ya nje, imani ya wawekezaji, uzalishaji na ajira katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya maua.

KFC ilihimiza pande zote (wahudumu wa matatu na serikali) kuweka mbele mazungumzo na kuhakikisha kuwa njia muhimu za usafirishaji na mizigo zinaendelea kufanya kazi ili kulinda mauzo ya nje ya Kenya, ajira na kulinda hadhi ya nchi katika soko la kimataifa.

Mgomo huo, hata hivyo, ulisitishwa kwa muda wa siku saba Jumanne, Mei 19, 2026 baada ya wamiliki wa matatu na wadauhusika kuafikiana na serikali, kuweka mikakati kutathmini bei ya mafuta ya petroli.

Ukuzaji maua nchini Kenya ni kati ya sekta kuu zinazoiingizia nchi fedha za kigeni, ikizalisha zaidi ya Sh110 bilioni kila mwaka huku ikitoa zaidi ya nafasi za ajira 200,000 za moja kwa moja na kusaidia zaidi ya watu milioni 1.5 kujipatia riziki kwa njia isiyo ya moja kwa moja.