Habari za Kitaifa

Duale: Tuko tayari kupambana na ugonjwa wa Ebola

Na WAANDISHI WETU  May 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI ya Kenya imeimarisha hatua za dharura za kukabiliana na Ebola huku ikiweka timu za wataalamu wa afya katika hali ya tahadhari saa 24 kufuatia mlipuko wa ugonjwa huo katika nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Uganda.

Waziri wa Afya, Aden Duale, alisema serikali imeanzisha mfumo wa kitaifa wa usimamizi wa dharura kupitia Taasisi ya Kitaifa ya Afya ya Umma, huku vituo vya operesheni za afya ya umma vikichukua tahadhari katika ngazi ya kitaifa na kaunti.

“Zaidi ya wasafiri 34,500 tayari wamefanyiwa uchunguzi katika vituo mbalimbali vya kuingia nchini, wakiwemo abiria wa kimataifa 18,552, wasafiri wa ndani 5,848, madereva wa malori 2,514 na vyombo vya usafiri 4,729,” alisema Bw Duale.

Alisema mfumo wa mtandaoni wa kufuatilia wasafiri unatekelezwa huku serikali ikiendelea kutambua mienendo ya watu katika maeneo yaliyo katika hatari kubwa mpakani.

Maabara maalum za kupima Ebola zimeandaliwa katika vituo vya KEMRI Kisumu, KEMRI Nairobi, Maabara ya Kitaifa ya Afya ya Umma.

Serikali pia imeimarisha ushirikiano na serikali za Uganda na DRC, Shirika la Afya Duniani (WHO), Jumuiya ya Afrika Mashariki na Kituo cha Magonjwa Afrika (CDC Africa).

“Hakuna kisa cha Ebola kilichothibitishwa nchini Kenya kuhusiana na mlipuko wa sasa. Hata hivyo, kutokana na uhusiano mkubwa wa usafiri kati ya Kenya na mataifa jirani, serikali imeimarisha ufuatiliaji na maandalizi nchini kote,” alisema Bw Duale.

Kaunti kadhaa zimeanza maandalizi ya kukabiliana na visa vinavyoweza kujitokeza.

Turkana imeandaa Hospitali ya Kanam Kemer kushughulikia visa vinavyoshukiwa huku vituo vya kutenga wagonjwa vikianzishwa Lokiriama, Nadapal na Kalobeyei.

Kw aupande mwingine, Busia imeongeza ukaguzi katika mipaka ya Busia na Malaba, huku Homa Bay ikipeleka maafisa wa afya katika maeneo ya Sena na Mbita kandokando ya Ziwa Victoria.

Nakuru nayo imetajwa kuwa eneo la hatari kutokana na kuwa kitovu cha usafiri kinachohudumia zaidi ya kaunti sita jirani.

Hata hivyo, baadhi ya kaunti zimekiri kuwa miundombinu iliyotumika wakati wa janga la corona imevunjwa au kubadilishwa matumizi, hali inayotatiza maandalizi ya sasa.

Mlipuko huo unahusisha aina ya Bundibugyo, mojawapo ya aina hatari zaidi za Ebola ambayo haina chanjo wala tiba iliyoidhinishwa.

Dalili za awali ni homa, maumivu makali ya kichwa, uchovu kupita kiasi na macho kuwa mekundu.

Kadri ugonjwa unavyoendelea kusambaa, mgonjwa anaweza kupata maumivu makali ya koo, kifua na tumbo pamoja na kutapika na kuharisha.

Maafisa wa afya wamewahimiza Wakenya kunawa mikono mara kwa mara, kuepuka kugusa wagonjwa au majimaji ya mwili ya aliyeambukizwa na kutafuta matibabu haraka wakionyesha dalili hizo, hasa baada ya kusafiri Uganda au mashariki mwa DRC.