Habari

Mahakama yatoa uamuzi wa kihistoria kuhusu mzozo wa ardhi jijini Nairobi

Na JOSEPH WANGUI July 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAMANI ya eneo iliyochorwa katika miaka ya 1980 ilitelekezwa kwa zaidi ya miongo mitatu kabla ya kujitokeza kuwa moja kati ya sakata kubwa zaidi kuhusu ardhi nchini.
Kilichoanza kama mradi maalum wa makazi ya kibinafsi katika eneo la Kaskazini mwa Nairobi, kiligeuka kesi ya kulipwa fidia ya ShSh3.2 bilioni iliyovutia tume za kikatiba, wapelelezi wa kupiga vita ufisadi na korti, huku maafisa waking’ang’ana kujibu swali moja: Ni nani hasa alimiliki ardhi iliyojengwa shule mbili za umma?
Wengine waliovutwa kwenye kashfa hiyo ni aliyekuwa waziri wa elimu, Fred Matiang’i baada ya wizara yake kukubali ushauri kutoka kwa Tume ya Ardhi Nchini (NLC) na kulipa awamu ya Sh1.5 bilioni ili kumiliki ardhi hiyo, ikibakisha salio la Sh1.7 bilioni.
Kiini cha mzozo huo ni ekari 13.7 zilizojengwa Shule ya Msingi ya Drive-In na Shule ya upili ya Ruaraka High.
Mzozo huo ulianza Disemba 1981 katika enzi ya Tume ya Jiji la Nairobi, jiji kuu lilipokuwa likipanuka kwa kasi huku wastawishaji wakifungua maeneo mapya ya ustawishaji.
Kampuni za Afrison Export Import Limited na Huelands Limited zilinunua ardhi iliyosajiliwa kama LR No. 7879/4, yenye ekari 96 kutoka kwa kampuni kwa jina Joreth Limited.
Ilichukua vilevile mkopo wa Sh21 milioni kutoka shirika la Continental Credit Finance Limited (lililofilisika) kufadhili ujenzi wa majumba 500 yenye ghorofa moja ya Kampuni ya Posta na Mawasiliano (KPTC).
Rekodi za korti zilionyesha ustawishaji huo ulipangiwa kujumuisha takriban nyumba 1,200 ikiwemo barabara, mifereji ya majitaka, duka, vituo vya kijamii na ardhi iliyohifadhiwa kwa taasisi za umma, ikiwemo shule ya msingi na ya sekondari.
Francis Mburu, mkurugenzi wa Afrison Export Import Ltd na Huelands Ltd, alieleza korti kampuni ilikataa masharti ya mpangilio kwa sababu, kwa maneno yake, “yalikuwa makali na yasiyoweza kutimizwa kifedha.”
Mvutano huo uliingia awamu mpya 2015 wakati Bw Mburu aliwasilisha kesi ya kihistoria kuhusu ukiukaji wa haki kuhusu ardhi kwa NLC.
Korti ya rufaa iliunga mkono uamuzu kuwa ardhi ya shule ilijumuisha sehemu ya ardhi iliyotengewa shughuli za umma na kukataa jaribio la wastawishaji kubatilisha uamuzi wa korti ya Mazingira na Ardhi.
Uamuzi huo pia ulizima ombi lao la kudai Sh1.76 bilioni walizohoji zilisalia baada ya malipo ya kwanza ya Sh1.5 bilioni.
“Tumebaini kuwa shule hizo zipo kwenye ardhi ya umma kwani NlC haikuwa na msingi kisheria wa kuitwaa kwa lazima, walisema majaji wa korti ya
Walibaini kuwa mpango wa makazi uliidhinishwa na walalamishi wakawezesha ujenzi wa nyumba 196 za GSU kuambatana na mradi ulioidhinishwa.
“Ushahidi uliorekodiwa vilevile unathibitisha usalimishaji bayana. Barua ya Julai 4, 1984 kutoka kwa wakala wa walalamishi kinathibitisha hali ya kuafikiana kuhusu usalimishaji huu,” walisema majaji.