Katibu Fikirini akiri jinsi Joho, Raila walivyomsaidia kupata kazi
RAIS William Ruto amesisitiza kujitolea kwa serikali yake kuhakikisha vijana wanapata nafasi ya kuchangia kwa maendeleo ya nchi.
Akizungumza katika eneo la Ganze wakati wa ibada ya shukrani ya Katibu wa Wizara ya Vijana, Bw Fikirini Jacobs, Rais alieleza jinsi aliyekuwa kinara w ODM, hayati Raila Odinga, alivyompendekeza katibu huyo licha ya kuwa na umri wa miaka 28.
Rais alikiri kwamba kwa kawaida, wadhifa wa Katibu wa Wizara umekuwa ukipewa watu ambao wamehudumu kwa karibu miaka 20 katika utumishi wa umma.
Aliamua kumpa Bw Jacobs nafasi akawa ndiye Katibu mwenye umri mdogo zaidi katika serikali, na tangu alipoajiriwa mwaka uliopita amedhihirisha uwezo wake.
“Hii ni ishara ya imani yetu kwamba vijana pia wanaweza kuchangia maendeleo ya taifa letu,” alisema Rais.
Katibu huyo alifichua jinsi alivyopigiwa simu na Waziri wa Madini na Uchumi wa Baharini, Bw Hassan Joho, kutuma ombi la wadhifa huo.
Wakati huo, alikuwa amefanya kazi kwa mwaka mmoja unusu pekee katika Serikali ya Kaunti ya Kilifi, baada ya kuhitimu kutoka Chuo Kikuu cha Pwani.
“Joho alinipigia simu kuniambia kuna kazi zinakuja hapa mbele nisikae mbali, nikamwambia sina tajriba ya kutosha, akasema tajriba ya mwaka mmoja unusu imetosha, jaribu mengine tutaangalia hapo mbele,” akaeleza.
Wakati huo huo, rais ameagiza hifadhi ya kijamii ya wanyama ya Shirango ifungwe mara moja, kufuatia malalamiko ya wakazi na viongozi kwamba imechangia ongezeko la mashambulio ya ndovu vijijini.
Aliamrisha kibali cha hifadhi hiyo kifutiliwe mbali, na ardhi irudishiwe wananchi.
“Serikali itahakikisha hamtasumbuliwa tena na wale walioandikisha hifadhi hiyo bila nyinyi kujua,” akawaambia wakazi.
Wakazi wa maeneo mengi ya Kilifi wamekuwa wakilalamikia uharibifu, majeraha na hata vifo vinavyosababishwa na wanyamapori wanaovamia vijiji vyao kila mara.
Tatizo kubwa zaidi limekuwa la ndovu, ambapo mamia ya wanyama hao huondoka katika mbuga za Tsavo na kuhangaisha wananchi huku wakiharibu mashamba.
Mbali na Kilifi, madhara yamekuwa yakitokea sana pia katika Kaunti za Taita Taveta na Kwale.
Rais Ruto amekuwa kwenye ziara ya maendeleo ya siku tano katika eneo la Pwani tangu Alhamisi iliyopita.
Akizungumza katika hafla ya Jumapili, Dkt Ruto aliwahimiza Wakenya wote kujisajili katika Mamlaka ya Afya la Jamii (SHA).
Alisema usajili huo ni muhimu ili serikali ipate takwimu sahihi za sekta ya afya na kuchukua hatua zinazofaa pale inapohitajika.
“Ninawaomba wote wajisajili SHA ili tuwe na takwimu sahihi. Tunataka kila Mkenya aweze kwenda hospitali na asiulizwe pesa kwa sababu SHA itaweza kulipa,” alisema.
Kwa mujibu wa takwimu za hivi karibuni, karibu Wakenya milioni 29 wamesajiliwa kwenye bima hiyo ya afya, lakini ni milioni tano pekee wanaochangia kikamilifu.
Rais pia alisisitiza wito wake wa siasa zisizotenganisha wananchi kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Aliwakosoa wanasiasa wanaoendelea na siasa za uchochezi, akiwataka viongozi kuzingatia kutoa suluhisho la changamoto zinazokumba nchi badala ya kueneza chuki.
Wakati wa ziara yake Pwani kufikia sasa, Rais ameongoza uzinduzi wa miradi iliyokamilika na kuanzisha mingine mipya ikiwemo barabara, masoko na miradi ya uchumi wa baharini kunufaisha wavuvi.
Vilevile, alisisitiza kuendeleza mpango wa kununua mashamba kutoka kwa mabwanyenye wasioyatumia ili kukabidhi maskwota hatimiliki.