Pigo tamasha la Kanye West Italia likipigwa marufuku
MAMLAKA nchini Italia zimepiga marufuku tamasha mbili zilizopangwa kufanyika Julai katika mji wa Reggio Emilia na wanamuziki wa rapa wa Amerika, Kanye West na Travis Scott.
Uamuzi huo ulitangazwa Jumamosi na mkuu wa serikali katika eneo hilo, Salvatore Angieri, ambaye alisema tamasha hizo zimefutwa kutokana na wasiwasi kuhusu usalama pamoja na uwezekano wa maandamano.
Scott alifaa kutumbuiza katika Tamasha la Pulse of Gaia Julai 17 katika ukumbi wa RCF Arena huku Kanye West, anayejulikana pia kama Ye, akitarajiwa kutumbuiza watu siku iliyofuata.
Kanye amekuwa akiandamwa na kufutwa kwa matamasha kadhaa barani Ulaya katika miezi ya hivi karibuni kufuatia matamshi yake ya kupinga Wayahudi.
Mwanamuziki huyo amewahi kutoa kauli za kumsifu dikteta wa Ujerumani wa zamani, Adolf Hitler, na kuchapisha maudhui yaliyohusishwa na alama za msimamo wake dhidi ya Wayahudi.
Matamshi hayo yalikosolewa na mashirika ya kutetea haki za binadamu na jumuiya za Wayahudi duniani.
Kwa upande wake, Travis Scott ameendelea kukumbwa na maswali kuhusu usalama katika matamasha yake tangu tukio la mwaka 2021 katika tamasha la Astroworld mjini Houston, Texas, ambapo watu 10 walifariki na mamia kujeruhiwa baada ya umati mkubwa kusongamana.
Angieri alisema uamuzi wa kufuta matamasha hayo ulifikiwa baada ya maombi kutoka kwa kundi moja pamoja na jumuiya ya Wayahudi katika mikoa ya Modena na Reggio Emilia, ambao walieleza wasiwasi wao hasa kuhusu ushiriki wa Kanye.
Mamlaka pia zilisema kuwa muda mfupi kati ya tamasha hizo mbili na idadi kubwa ya mashabiki waliotarajiwa kuwasili ndani ya saa 24 uliongeza hatari za kiusalama.
Aidha, walitaja kufutwa kwa matamasha mengine ya Kanye katika mataifa mbalimbali ya Ulaya kama “hatari halisi” ya maandamano makubwa dhidi ya mwanamuziki huyo.
Hatua hiyo ni pigo jingine kwa Kanye, ambaye amekuwa akipoteza nafasi za kutumbuiza katika mataifa kadhaa kutokana na kauli zake zenye utata, huku mijadala ikiendelea kuhusu mipaka ya uhuru wa kujieleza na wajibu wa wasanii maarufu kwa jamii.