Dimba

Amenya amzidi nguvu Hakim kwa TKO, Jin Shen ang’aa mashindano ya ndondi ya Rising Stars

Na TOTO AREGE May 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JASHO, presha na shamrashamra zilitawala katika toleo la tatu la mashindano ya Ndondi ya Rising Stars yaliyoandaliwa katika viwanja vya ASK Showground, Jamhuri jijini Nairobi Ijumaa.

Mashindano hayo ya mapambano nane yaliyodhaminiwa na kampuni ya SportPesa na kuandaliwa na Maurice Odera kupitia Ultra Fight Series Boxing (UFS BXNG), yaliwashuhudia mabondia wakionyesha uwezo mkubwa huku Technical Knockouts (TKO) zikitoa burudani ya kiwango cha juu kwa mashabiki waliofurika ukumbini.

TKO inamaana, kumalizika kwa mapambano kwa uamuzi wa kiusalama au wakati bondia anatupa taulo ndani ya ukumbi au kuomba pambano lisimamishwe.

Pambano kuu kati ya Amos Amenya na Abdul Hakim lilikuwa kali kuanzia mwanzo hadi mwisho huku mabondia hao wawili wakibadilishana makonde na mbinu za kila aina kutafuta ushindi.

Mapambano hayo yaliendelea hadi raundi ya sita kabla ya Amenya kumpiga Hakim kwa TKO na kutwaa ushindi katika pambano la uzani wa Super-Featherweight.

Meneja wa Ushirikiano na Udhamini wa SportPesa, Japheth Akhulia, alisema moja ya vitu vinavyofanya mashindano hayo kuwa ya kipekee ni uwiano wa uwezo kati ya mabondia wanaoshiriki.

“Kitu cha kipekee kuhusu SportPesa Boxing Rising Stars ni uwiano wa nguvu kati ya mabondia. Wale wanaokutana ulingoni huwa na nafasi sawa ya kuonyesha vipaji vyao,” alisema Akhulia.

Aliwahimiza mashabiki kujitokeza kwa wingi kushuhudia mapambano hayo akisema, baadhi ya mabondia wanaoshiriki wana nafasi kubwa ya kuwa mastaa wa baadaye katika mchezo wa ndondi.

Kauli yake iliungwa mkono na Mkuu wa Udhamini wa Kimataifa wa SportPesa, Alan McTavish, aliyesema walipanga kalenda ya mwaka 2026 kuhakikisha kuna mchanganyiko wa mashindano ya chipukizi pamoja na mashindano mengine.

Wakati huo huo, bondia Jin Shen mwenye umri wa miaka 21 aliendelea kung’ara baada ya kumwangusha Elias Njoroge kupitia TKO katika raundi ya pili ya pambano lao la Bantamweight.

Shen alipata ushindi wake wa pili mfululizo katika mashindano hayo baada ya kufanya vizuri pia kwenye mchezo wake ya kwanza Februari mwaka huu alipomshinda Jeremiah Abuko.

“Niliweza kumshinda Njoroge kutokana na mazoezi mazuri ya nguvu na maandalizi makali niliyofanya,” alisema Shen.

Aliongeza kuwa analenga kuendelea na kiwango hicho huku akiimarisha jina lake katika mchezo wa ndondi.

 Matokeo ya Mapambano

  1. Welterweight (Raundi 4)

Edwin Hayo alimshinda Moses Siviya

Alama: 39-37, 38-38, 39-37

2.Super Lightweight (Raundi 4)

McGregor Njoroge alimshinda Davis Gwaro

Kwa TKO ((Raundi ya 3)

3.Featherweight (Raundi ya 4)

John Logova alimshinda Muiruri Irungu

Kwa TKO (raundi ya 1)

  1. Light Heavyweight (Raundi ya 4)

Gentry Ochieng alimshinda Peter Wanda

Kwa TKO ((Raundi ya 2)

  1. Lightweight (Rounds 4)

Victor Oduor Andere alimshinda Dennis Ashley

Alama: 40-36, 39-36, 40-36

  1. Bantamweight (Raundi ya 4)

Jin Shen alimshinda Elias Njoroge

Kwa TKO (raundi 2)

7.Light Heavyweight (Raundi 4)

Elijah Kingi alimshinda James Otieno

Kwa TKO (raundi ya 1)

  1. Super Featherweight (Raundi ya 6)

Amos Amenya alimshinda Abdul Hakim

Kwa TKO (raundi ya 6)