Kenya kuwa mwenyeji wa mashindano ya UFAK ya Karate
Shirikisho la Karate Nchini (KKF) linaandaa Mashindano ya Karate ya Mkoa wa Mashariki 2026, yatakayo fanyika kuanzia tarehe 28 hadi 31 mwezi huu katika ukumbi wa ndani wa uwanja wa Nyayo jijini Nairobi.
Mashindano hayo yanayoandaliwa chini ya mwavuli wa Muungano wa Shirikisho la Karate la Afrika (UFAK), yanatarajiwa kuvutia wanakarate bora, makocha, waamuzi, maafisa na wajumbe kutoka mataifa 14 ya Afrika Mashariki katika tamasha litakaloonyesha ustadi, nidhamu, umoja na ubora wa michezo.
Kwa siku nne, jiji la Nairobi litageuka kitovu cha mchezo wa karate Afrika huku washindani wa kitengo cha cadet, junior na senior wakishindana.
Nahodha wa timu ya Kenya Francis Wamukui alisema wana matumaini makubwa ya kuibuka mabingwa mwaka huu baada ya kumaliza wa pili mwaka jana.
“Tulimaliza katika nafasi ya pili mwaka jana na safari hii tumejipanga vizuri kutwaa ubingwa. Mafunzo tuliyopata kambini na kiwango cha ukocha kimetuimarisha sana. Pia kucheza nyumbani ni motisha kubwa na hatutaki kushindwa mbele ya mashabiki wetu,” alisema Wamukui.
Kenya itaingia mashindanoni ikiwa na kikosi cha wanariadha 50 waliochaguliwa kupeperusha bendera ya taifa nyumbani.
Timu hiyo imekuwa kambini baada ya kukamilisha mazoezi makali ya miezi miwili chini ya makocha walioidhinishwa na Shirikisho la Karate Duniani (WKF), huku wakisisitiza mbinu za kiufundi, utimamu wa mwili, nidhamu na umakini wa mchezo.
Timu ya Kenya inaingia mashindanoni kwa kujiamini baada ya kufanya vizuri nchini Ethiopia mwaka jana ilipomaliza ya pili kwa jumla nyuma ya wenyeji kwa kujinyakulia medali 20 dhahabu 10, fedha tisa na shaba moja.
Shirikisho linaamini faida ya kucheza nyumbani pamoja na maandalizi ya kutosha yanaweza kusaidia Kenya kuvunja rekodi hiyo na kutwaa ubingwa wa jumla.
Wakili Mercy Wamboi pia ataiwakilisha Kenya katika mashindano hayo na amewataka Wakenya kujitokeza kwa wingi kuipa timu sapoti.
“Kuna mtazamo kuwa karate ni mchezo wa wanaume pekee, lakini ukweli ni kwamba wanawake kambini ni wengi kuliko wanaume.
Hatuko hapo kujaza nafasi bali kushindana na kufanya vizuri. Mashindano haya yatawafungua macho wengi, hivyo Wakenya wajitokeze kuishangilia Kenya,” alisema Wamboi.
Mashindano ya Nairobi pia yatahudhuria viongozi mashuhuei wa karate duniani akiwemo Rais wa karate Afrika, Makamu Rais wa WKF, Mwenyekiti wa Kamati ya Waamuzi ya WKF, Mwenyekiti wa Kamati ya Waamuzi ya UFAK pamoja na Mkuu wa Kamati ya Kiufundi ya UFAK, jambo linalodhihirisha jinsi Kenya inavyoendelea kujijengea jina kama mwenyeji wa matukio makubwa ya kimataifa ya michezo.
Mbali na ushindani mkali, mashindano hayo pia yatatumika kukuza mchezo wa karate Afrika kupitia kozi maalum za makocha na waamuzi, semina pamoja na mitihani ya kuongeza viwango vya utaalamu barani humo.
Mashindano hayo pia ni sehemu ya maandalizi ya Kenya kuelekea mashindano ya Afrika ya karate yatakayofanyika Algeria Septemba na Michezo ya Jumuiya ya Madola nchini Scotland Oktoba mwaka huu.
Afisa wa Shirikisho la Karate Kenya Mhandisi Richard Binga aliishukuru serikali kwa msaada wake katika maandalizi ya mashindano hayo.