Nanjala aipa Starlets matumaini ya kutinga Kombe la Dunia
ZIKIWA zimesalia siku nne kabla ya kuanza kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) 2026, mshambuliaji wa Harambee Starlets Violet Nanjala anaamini Kenya inaweza kufuzu kwa Kombe la Dunia la Wanawake mwakani nchini Brazil kwa mara ya kwanza.
Makala hayo ya 16 ya michuano hiyo, yatanza rasmi Jumapili hii hadi Agosti 16 nchini Morocco.
Kenya imepangwa kundi gumu Kundi A pamoja na wenyeji Morocco, Senegal na Algeria. Starlets wataanza kampeni yao dhidi ya Morocco Jumapili hii, kabla ya kuvaana na Senegal Julai 30 kisha watahitimisha mechi za hatua ya dhidi ya Algeria Agosti 3.
“Tuko tayari kwa mashindano haya na lengo letu ni kufuzu Kombe la Dunia. Inawezekana kwa sababu tumefanyia kazi makosa yetu na naamini tumejiandaa vya kutosha,” alisema Nanjala.
Aliongeza kuwa kuahirishwa kwa mashindano hayo kuliipa timu muda wa kuboresha maeneo yaliyokuwa na udhaifu.
Nanjala anaelekea Morocco akiwa amejawa na furaha baada ya kutimiza ndoto yake ya kucheza Ulaya kufuatia kusajiliwa na Hibernians FC ya Ligi Kuu ya Wanawake nchini Malta akitokea United Eagles Women FC ya Saudi Arabia.
Hibernians ilimtaja Mkenya kuwa, mshambuliaji mwenye kasi na uwezo wa kucheza nafasi mbalimbali katika safu ya ushambuliaji.
Nanjala, 26 alijiunga na United Eagles msimu uliopita baada ya kuitumikia Municipal de Laayoune ya Morocco kwa misimu mitatu.
Pia, ni mchezaji wa zamani wa Trans Nzoia Falcons katika Ligi ya Kitaifa ya Wanawake na Vihiga Queens mabingwa mara nne wa Ligi Kuu ya Wanawake (KWPL).
Akizungumzia uhamisho wake mpya, Nanjala alisema ni hatua muhimu katika taaluma yake.
“Hii ni nafasi kubwa kwangu kujipima barani Ulaya. Ninaamini uwezo wangu na ninajua nilikotoka. Nimefurahi kwa sababu nilifanya kazi kwa bidii kupata nafasi hii na naamini nitafanikiwa. Kucheza katika mojawapo ya ligi bora Ulaya imekuwa ni ndoto yangu,” alisema shabiki huyo wa Manchester United.
Kikosi cha wachezaji 24 cha Starlets kitaondoka Alhamisi kutoka kambi yao ya Miramas kusini mwa Ufaransa kuelekea Morocco baada ya kukamilisha kambi ya wiki moja ya maandalizi.
WAFCON pia ni mashindano ya kufuzu Kombe la Dunia la Wanawake. Timu nne zitakazofuzu nusu-fainali zitajikatia tiketi ya moja kwa moja huku timu mbili nyingine zikielekea kwenye mchujo wa mabara mbalimbali kuwania nafasi zilizosalia.