Wakulima wa avokado Kiambu wanufaika na masoko ya nje
KATIKA Kijiji cha Cura, Kiganjo, Gatundu Kusini, Kaunti ya Kiambu, wakulima wa maparachichi wameanza kuandikisha mabadiliko makubwa baada ya miaka mingi ya kupunjwa na madalali waliokuwa wakidhibiti bei na mara nyingine kutowalipa.
John Mburu Ndotono, aliyeingilia kilimo cha maparachichi, maarufu kama avokado, mwaka 2016 baada ya kuacha ufugaji wa ng’ombe wa maziwa, anakumbuka changamoto hizo kwa uchungu.
Anasema alipoanza kukuza matunda hayo, mabroka walikuwa wakiyanunua kwa bei ya kutupa.
“Dalali angenunua kwa kati ya Sh3 na Sh5 kwa kilo. Wakati mmoja walivuna kilo 1,500 katika shamba langu na kuahidi kurudi kuchukua matunda baadaye, lakini hawakurudi kamwe,” anaelezea kwa huzuni.
Matunda hayo yaliozea shambani, na kusababisha hasara kubwa.
Lucy Mumbi, mkulima mwingine, naye anakumbuka kuuza maparachichi kwa Sh2.50 kwa tunda.
“Baadhi ya madalali walipakia kwenye lori na kutoweka bila kulipa. Mkulima hakuwa na mamlaka yoyote,” Mumbi anakumbuka.
Kwa sababu ya ukosefu wa miundomsingi faafu, hasa mifumo ya baridi kuhifadhi avokado, wakulima walilazimika kuuza mazao mara moja baada ya kuvuna ili kuepuka kuharibika. Hadi asilimia 50 ya mazao yalikuwa yakipotea, hasa msimu wa mavuno mengi.
Mkulima mwingine, James Mwangi Kibunja, anasema udanganyifu haukuishia kwenye bei pekee.
“Broka angesema anachukua matunda matano lakini anaongeza mawili zaidi bila wewe kujua,” anaeleza.
Hata hivyo, hali hiyo sasa inabadilishwa na kampuni ya Soko Fresh kupitia mfumo wa baridi unaotumia nguvu za umeme na nishati ya jua.
Kampuni hiyo imeunganisha wakulima wa mashamba madogo na masoko ya kimataifa.
“Tuligundua kuwa asilimia 80 ya uzalishaji wa maparachichi nchini inatoka kwa wakulima wa mashamba madogo, lakini masoko ya kuuza nje ya nchi yanatawaliwa na wamiliki wa mashamba makubwa. Lengo letu ni kuwajumuisha wakulima hawa katika mitandao yenye thamani kubwa,” anasema Stephen Katingima, Afisa Mkuu wa Mikakati Soko Fresh.
Kampuni hiyo inafanya kazi na zaidi ya wakulima 15,000 na imeanzisha zaidi ya vituo 32 vya kuhifadhi avokado kupitia mifumo ya baridi. Mfumo huo huongeza ubora wa matunda kwa hadi asilimia 20 na kupunguza upotevu baada ya mavuno.
Leo hii, Ndotono hupata kati ya Sh80 na Sh100 kwa kilo, ikilinganishwa na Sh3 hadi Sh5 alizokuwa akipata hapo awali.
“Sasa nina soko la uhakika. Hilo limebadilisha kila kitu,” akaambia Akilimali wakati wa mahojiano shambani mwake.
Alice Wangari, mkulima, alidokeza kwamba malipo hufanyika ndani ya dakika 30 baada ya kuwasilisha mazao.
Naye Doreen Khaule, ambaye ana zaidi ya miparachichi 200 katika ekari moja, sasa hupata karibu Sh90 kwa kilo badala ya Sh6 hadi Sh10 alizokuwa akilipwa hapo awali.
“Avokado sasa ni zao lenye thamani. Ninaweza kusomesha watoto wangu,” anasema.
Kulingana na Katingima, mwaka uliopita Soko Fresh ilisafirisha tani 300 za maparachichi nje ya nchi na kuhudumia takriban wakulima 5,000. Avokado bora huuzwa kwa Dola 1.9 hadi 2.1 (takriban Sh250–Sh280) kwa kilo, huku mkulima akipata hadi Sh120 kulingana na ubora.
Mafanikio hayo yamechangiwa pia na ufadhili wa Global Energy Alliance for People and Planet (GEAPP) kwa ushirikiano na CLASP. Kati ya mwaka 2021 na 2024, mpango wa mashirika hayo kuinua wakulima uliwekeza Dola milioni 6.1 (Sh787.99 milioni) katika nchi sita za bara Afrika, ikiwemo Kenya.
“Tunapunguza hatari ya uwekezaji. Kampuni zikiandikisha matokeo, fedha zaidi hutolewa ili kusaidia upanuzi,” anasema Carol Koech, Makamu wa Rais wa GEAPP Afrika.
Hata hivyo, wakulima bado wanakabiliwa na changamoto za gharama kubwa za pembejeo, wadudu waharibifu, wizi wa mazao, gharama za uthibitishaji wa viwango vya kimataifa na mabadiliko ya tabianchi yanayosababisha mvua zisizotabirika.