MAONI: Sifuna ajue amekuwa mkubwa kuliko anavyodhania, achunge
SENETA wa Nairobi Edwin Sifuna ni kati ya watu ambao majina yao yanasakurwa mno katika mitandao nje na ndani ya Kenya baada ya kutifua vumbi kubwa la fikra za kimapinduzi nchini.
Ni mwanasiasa mchanga anayevutia hadhira na watu kutoka mbali na karibu.
Wakubwa wanamshangaa, wadogo wanamheshimu na rika zake wanampa gumba. Watu wamemwambia agombee Urais mwaka ujao.
ODM inayumbayumba kwa ajili, UDA inamwona kama kijana aliyechafua soko lake la ushirika na ODM: Edwin Sifuna Watenya.
Watu wameanza kujiita “Sifuna” watoto ambao hawajaanza kuenda dede wamesikia sauti ya Sifuna katika vyombo vya habari.
Sifuna mwenyewe amesema madhumuni yake ni kuhakikisha kuwa Rais Ruto hatunukiwi awamu nyingine kuongoza Kenya.
Kijana aliyezaliwa magharibi anaonekana kupiga siasa za mapambano. Baadhi wanasema ni kivuli cha aliyekuwa kiongozi wa ODM Raila Odinga.
Mkutano uliofanywa katika Kaunti ya Machakos haswa katika kituo cha biashara cha Mlolongo Jumapili iliyopita uliashiria kuwa wimbi la Sifuna ni kubwa kuliko anavyodhania mwenyewe ama wafuasi wake.
Walijaa watu kwa wingi kama mchanga wa bahari. Baadhi wanadhania kuwa si lazima Sifuna agande katika chama cha ODM.
Inawezekana kuna watu wanaomiliki vyama ambao wako radhi kumkabidhi hata bila malipo akitumie kwa shughuli za siasa 2027.
Historia hii inaweza kulinganishwa na uchaguzi mkuu wa 2002. Sehemu kubwa haikuwa inamuunga mkono Uhuru Kenyatta wa KANU.
Wengi waliamua ni Mwai Kibaki ndiye mkombozi. Akashinda kwa kura nyingi. Ulimwengu wote ukasema Kibaki tosha.
Utawala wa miaka 40 ya KANU ukazima ghafla. Inawezekana pia watu waseme Sifuna hadi mwisho.
Pengine hawatajali chama, watatazama uwezo wake wa kuikomboa nchi jinsi anavyosema mwenyewe ama kutaka tuamini hivyo.
Ila anahitaji mikakati zaidi wakati huu, majira ya uchaguzi na hapo baadaye ili ngoma yake iendelee kurindima.
Narc iliposhinda KANU, wakuu wa dola tofauti zikiwemo zile za kwanza ulimwenguni walijinasibisha na Rais Mwai Kibaki.
Rais Mstaafu wa Amerika Bill Clinton alipoulizwa angetaka kukutana na nani akasema Mwai Kibaki. Hata sasa watu wanajiita “wao ndio Sifuna.”
Hii ina maana Sifuna anaweza kushinda lakini asiingie kwa mtego kama wa NARC ambayo ilipata kiburi pindi iliposhika ngazi.
Baada miezi sita hivi wengi wakaichukia, ilipofika 2004 Uhuru Kenyatta aliyekuwa kakejeliwa awali akawa malaika kwa Wakenya wengi.
Mnamo 2005, serikali hiyo ilikosa makali na hata katiba iliyopendekezwa ikaangushwa na Wakenya.
Katika uchaguzi mkuu wa 2007 Kibaki alishinda kwa taabu. Sifuna akifaulu anahitaji mikakati yasimpate yaliyomkumba Kibaki.
Paul Nabiswa ni mhariri, NTV