Linda Mwananchi sasa waelekea Mlimani wakijijenga kuwa vuguvugu la kitaifa
KUNDI la Linda Mwananchi ndani ya chama cha ODM sasa linaelekeza juhudi zake katika maeneo ambayo kwa muda mrefu hayajawahi kuwa ngome za chama hicho huku likijaribu kujijenga kama vuguvugu la kitaifa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Kundi hilo linalohusishwa na Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, sasa linapanga kufanya mkutano mkubwa mjini Thika mnamo Juni 14 katika kile kinachoonekana kama jaribio la kuvunja mipaka ya kisiasa ya jadi na kupenyeza katika eneo lenye kura nyingi la Mlima Kenya.
Hatua hiyo inajiri huku kukiwa na uvumi kuhusu mazungumzo ya siri ya kuunda muungano mpana wa upinzani kwa lengo la kumenyana na Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027.
Kundi hilo linaonekana kujiamini baada ya kupata mapokezi mazuri katika eneo la Ukambani wikendi iliyopita, ambako lilifanya mikutano katika maeneo ya Mutituni, Machakos na Mlolongo.
Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa Linda Mwananchi kufanya shughuli zake nje ya maeneo yanayoonekana kuwa ngome za ODM.
Awali, kundi hilo lilikuwa limefanya mikutano Nairobi, Busia, Kakamega, Kajiado, Narok, Kisumu na Mombasa.
Seneta wa Vihiga, Godfrey Osotsi, alisema lengo la kundi hilo ni kuunganisha Wakenya kutoka maeneo yote ya nchi.
“Tunapanua shughuli zetu zaidi ya ngome za jadi za ODM. Baada ya Thika tunapanga kuelekea maeneo kama Meru na Eldoret,” alisema.
Maoni ya wachanganuzi kuhusu mkutano wa Thika
Wachambuzi wa siasa wanataja mkutano wa Thika kama hatua muhimu katika safari ya kundi hilo ya kujijenga kitaifa.
Mchambuzi wa siasa Dkt Joshua Wafula, anasema kuwa iwapo mkutano wa Thika utapata mafanikio sawa na yale yaliyoshuhudiwa katika maeneo mengine, basi itakuwa vigumu kwa wanasiasa wengine kupuuza ushawishi wa Linda Mwananchi katika hesabu za urais za 2027.
“Uamuzi wa kuanzia Thika ni wa kimkakati kwa sababu Mlima Kenya utaendelea kuwa eneo muhimu katika kuamua mshindi wa uchaguzi wa urais,” anasema.
Katika uchaguzi wa 2022, eneo la Mlima Kenya pamoja na Bonde la Ufa Kaskazini lilichangia karibu asilimia 63 ya kura zote zilizompa ushindi Rais Ruto dhidi ya aliyekuwa mgombea wa Azimio, Raila Odinga.
Kaunti 10 za Mlima Kenya zilimpa Dkt Ruto zaidi ya kura milioni 2.9, huku maeneo hayo yakiendelea kuongoza katika usajili wa wapigakura wapya kulingana na takwimu za Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).
Mikakati ya Linda Mwananchi pia inafuatia taarifa kwamba kuna mazungumzo ya kuunda muungano kati ya kundi hilo na viongozi wa upinzani wanaohusishwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.
Muungano huo unahusisha pia kinara wa Wiper, Kalonzo Musyoka, na naibu kiongozi wa chama cha Jubilee, Fred Matiang’i.
Katika mkutano wa Machakos, Seneta Sifuna alidokeza uwezekano wa viongozi wa upinzani kuungana chini ya tiketi moja ya urais.
“Iwapo Kalonzo atasimama peke yake anaweza kumshinda Ruto. Sifuna naye akisimama peke yake anaweza kushinda. Lakini ili kurahisisha kazi hiyo, ni lazima tuungane,” alisema.
Kauli hiyo imezua mijadala kuhusu nafasi ya Bw Sifuna katika siasa za kitaifa, hasa kwa kukosa kufafanua iwapo atalenga urais au kutetea tena kiti chake cha Seneta wa Nairobi.
Kura ya maoni iliyotolewa mwezi uliopita na shirika la utafiti la TIFA ilionyesha kuwa miongoni mwa wafuasi wa upinzani, tiketi ya Kalonzo-Sifuna ilikuwa miongoni mwa chaguo maarufu zaidi ikiwa na umaarufu wa asilimia 28, ikifuatia tiketi ya Kalonzo-Matiang’i iliyopata asilimia 31.
Mnamo Aprili, Linda Mwananchi ilitangaza mpango wa kufanya tathmini ya maeneo mbalimbali nchini ili kubaini masuala yanayowagusa wananchi wa kila eneo na kuunda sera zitakazowavutia wapigakura.
Mpango huo pia unahusisha kuanzishwa kwa kituo maalum cha kuratibu shughuli zake, kukusanya pesa, kuandaa mikakati ya kisiasa na kusimamia ujumbe wa kundi hilo.
Seneta Osotsi ndiye aliyeteuliwa kuratibu shughuli za kundi hilo katika jukumu linalofanana na lile la katibu wa kisiasa.
Timu hiyo itakuwa ikitoa mapendekezo kwa viongozi wakuu wa Linda Mwananchi kabla ya maamuzi ya mwisho kufanywa.