Gachagua: Bajeti ya 2026/2027 ni sumu kubwa
KIONGOZI wa Chama cha Democracy for the Citizens (DCP), Rigathi Gachagua, amepinga mapendekezo ya bajeti ya mwaka wa kifedha 2026/27 akisema yanalenga kuwaumiza wananchi.
Bw Gachagua alisema bajeti ya Sh4.82 trilioni na Mswada Fedha 2026 ni hatari na utaumiza wananchi, wafanyabiashara wadogo, wakulima, vijana na sekta muhimu za uchumi.
“Mswada wa 2026 unawatoza Wakenya ushuru na kuwaacha wakiwa masikini. Ni mswada wa mauaji ya kiuchumi na tishio kwa mwananchi wa kawaida,” alisema Bw Gachagua alipokuwa akizindua kile alichokiita bajeti mbadala katika makao makuu ya DCP.
Alishutumu serikali kwa kupatia kipaumbele kukopa na kutoza ushuru badala ya kuwekeza kwenye afya, elimu, kilimo na ajira.
“Kila siku serikali inakopa na kuongeza mzigo kwa wananchi. Hii si bajeti ya maendeleo bali ya mateso,” alisema.
Bw Gachagua alidai kuwa serikali inapanga kukopa zaidi ya Sh1.1 trilioni katika mwaka ujao wa kifedha, akionya kuwa deni la taifa limefikia Sh13 trilioni.
Alitaja sekta ya elimu, afya na kilimo kama zilizoathirika zaidi, akisema fedha zinazotengewa ni chache sana ikilinganishwa na mahitaji ya wananchi.
Kulingana naye, elimu imepatiwa asilimia 16.2, kilimo asilimia 2 na afya asilimia 3.5 licha ya ongezeko la makato kupitia Mamlaka ya Afya ya Jamii(SHA).
“Mustakabali wa watoto wetu uko wapi? Kwa nini serikali hii iko vitani na vijana wetu?” alihoji.
Katika sekta ya kilimo, alitaka kujua kwa nini serikali inapunguza bajeti ilhali mamilioni ya Wakenya wanategemea sekta hiyo.
Bw Gachagua pia alikosoa vikali Mswada wa Fedha 2026/27, akisema unaongeza ushuru mpya utakaowalemea wananchi licha ya serikali kushindwa kufikia malengo yake ya mapato.
Alipinga pendekezo la kutoza VAT ya asilimia 16 kwa malipo ya kidijitali, ongezeko la ushuru wa bidhaa za simu kutoka asilimia 10 hadi 25, pamoja na mabadiliko ya ushuru kwenye bidhaa za nishati ya jua na chakula cha mifugo.
“Ushuru huu utapandisha gharama kwa wafanyabiashara, shule, hospitali na wananchi wanaotegemea malipo ya simu,” alisema.
Aliongeza kuwa simu za mkononi ni hitaji la msingi katika elimu, biashara na ajira.
“Kenya haiwezi kujenga uchumi kwa kutoza ushuru pekee,” alisema.
Katika mpango wake mbadala wa uchumi, DCP inapendekeza kufutwa kwa ushuru wa nyumba, kupunguzwa kwa matumizi yasiyo ya lazima ya serikali, kudhibiti ukopaji na kuongeza bajeti ya kilimo na afya.
Kulingana naye, chini ya mpango huo, bajeti ya kilimo itapanda hadi Sh300 bilioni kutoka Sh97 bilioni, huku afya ikipewa Sh450 bilioni kutoka Sh167.4 bilioni.
Pia inapendekeza kupunguza matumizi ya utawala kutoka Sh354.9 bilioni hadi Sh250 bilioni, na kuelekeza fedha hizo kwenye uzalishaji wa chakula, afya, elimu na ajira kwa vijana.
Bw Gachagua alihitimisha kwa kuwataka Wabunge kukataa bajeti hiyo na Mswada wa Fedha 2026, akisisitiza kuwa Kenya inapaswa kujenga uchumi unaojitegemea bila kuongeza deni jipya.