Habari

Onetam! Keter ajiunga na Linda Mwananchi ngome ya Ruto ikichemka

Na BARBANAS BII June 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

ALIYEKUWA Mbunge wa Nandi Hills, Alfred Keter, ameinuka tena kisiasa baada ya kipindi kirefu cha ukimya, akilenga kuvuruga ushawishi wa chama cha UDA kinachoongozwa na Rais William Ruto katika eneo la Bonde la Ufa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Bw Keter, ambaye amekuwa mkosoaji mkubwa wa Rais Ruto, sasa ameungana na mrengo wa Linda Mwananchi unaohusishwa na Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna.

Wachambuzi wa siasa wanachukulia hatua hiyo kama juhudi za kuunda muungano madhubuti wa upinzani dhidi ya Rais Ruto katika ngome yake ya kisiasa.

“Tunalenga kujenga nguvu mpya ya kisiasa itakayomnyima Rais William Ruto usingizi. Ninawasihi wakazi wa Bonde la Ufa wapige kura kwa kuzingatia dhamiri zao,” alisema Bw Keter.

Kurejea kwake katika siasa kunafuatia mvutano wa muda mrefu kati yake na viongozi wa kisiasa wanaomuunga mkono Rais Ruto, hali iliyochangia kushindwa kwake katika mchujo wa UDA kabla ya uchaguzi wa mwaka 2022.

Bw Keter alidai kuwa mchakato huo ulikumbwa na dosari nyingi.

Alichaguliwa Mbunge wa Nandi Hills mwaka 2013 na akahifadhi kiti hicho mwaka 2017 kupitia chama cha Jubilee.

Hata hivyo, alikosa tiketi ya UDA mwaka 2022 na akagombea kama mgombea huru lakini akashindwa na Bernard Kitur wa UDA.

Katika uchaguzi huo, Bw Keter alipata kura 18,037 dhidi ya kura 23,503 za Bw Kitur katika pambano lililotafsiriwa kama mtihani wa nguvu kati ya Rais Ruto na wagombea huru katika eneo hilo.

Kwa kuwa Rais Ruto anachukuliwa kuwa kiongozi mkuu wa jamii ya Kalenjin, Bw Keter ametajwa mara kwa mara kama mwanasiasa muasi anayepinga juhudi za rais kupata muhula wa pili.

Mwanasiasa huyo ameshutumu serikali ya Kenya Kwanza kwa kushindwa kushughulikia changamoto za kiuchumi zinazowakabili Wakenya wa kawaida.

Aidha, amedai kuwa ufisadi na usimamizi mbovu umeathiri sekta muhimu za uchumi.

“Serikali ya sasa imefanya machache kuboresha maisha ya Wakenya. Nimeungana na viongozi wenye mawazo kama yangu akiwemo Edwin Sifuna, Babu Owino na wengine ili kuikomboa nchi,” alisema katika mahojiano ya simu.

Licha ya uvumi kuhusu mustakabali wake wa kisiasa, Bw Keter amesema hana nia ya kuwania kiti chochote mwaka 2027.

Badala yake, amesema lengo lake kuu ni kusaidia upinzani dhidi ya azma ya Rais Ruto kutafuta muhula wa pili.

“Sina uhasama wa kibinafsi na Rais Ruto. Tatizo ni kwamba hatukubaliani kuhusu masuala yanayowahusu wananchi na taifa kwa jumla. Ndiyo maana naamini hastahili muhula mwingine,” alisema.

Bw Keter alisema kundi lake limepanga kufanya mikutano ya kisiasa katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwemo Meru na Eldoret, ili kueneza ujumbe wao.

“Siasa zetu zinazingatia masuala yanayowagusa wananchi. Tunataka kuhoji utendaji wa serikali kuhusu matatizo yanayokumba karibu kila sekta ya uchumi,” alisema.

Alitaja sekta ya kilimo kama mojawapo ya zilizopuuzwa, akisema wakulima wa chai wanapata bonasi ndogo huku wakikumbwa na gharama kubwa za uzalishaji. Aidha, alisema wakulima wa nafaka wanapata ugumu wa kupata mbolea ya kukuzia mimea huku bei ya mafuta ikiendelea kupanda.

“Sekta ya elimu pia imeathirika, jambo linalodhihirika katika matatizo ya kifedha yanayokumba Chuo Kikuu cha Moi. Sekta ya afya nayo iko katika hali mbaya,” alisema.

Pia, alikosoa serikali kwa kile alichokitaja kuwa kasi ndogo ya kufufua kampuni ya nguo ya Rivatex mjini Eldoret baada ya kukodishwa kwa mshirika wa kibinafsi kwa miaka 21.

Wakati huo huo, hali ya kisiasa katika Kaunti ya Uasin Gishu inaendelea kuwa tete huku viongozi wa UDA wakizozania masuala ya usimamizi wa rasilimali za umma na mwelekeo wa kisiasa kuelekea uchaguzi wa 2027.

Makundi yanayomuunga mkono Seneta Jackson Mandago na Gavana Jonathan Bii yamekuwa yakitupiana lawama kuhusu matumizi ya fedha za maendeleo na utekelezaji wa miradi ya umma.

Mbunge wa Soy David Kiplagat na mwenzake wa Kesses Julius Ruto wameungana na Seneta Mandago kumshutumu Gavana Bii kwa madai ya matumizi mabaya ya fedha za maendeleo na kuchelewesha miradi mbalimbali. Hata hivyo, gavana huyo amekanusha madai hayo.

Kwa upande wake, Gavana Bii amewashutumu wakosoaji wake kwa kukosa uaminifu kwa UDA na kuhusishwa na viongozi wanaomuunga mkono kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua.

“Hata kama hunitaki, tathmini maendeleo ambayo nimeleta na umuunge mkono rais wetu kupata muhula wa pili,” alisema Bw Bii.