Habari za Kaunti

Gavana Nassir ajikuta pabaya baada ya ahadi zake kuu kugonga ukuta

Na WINNIE ATIENO June 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

GAVANA wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, anakabiliwa na changamoto ya kutekeleza ahadi alizotoa wakati wa kampeni huku Uchaguzi Mkuu wa 2027 ukikaribia.

Wakati alipochaguliwa kuwa gavana mwaka wa 2022, Bw Nassir aliahidi mageuzi makubwa katika huduma za afya na elimu.

Bw Nassir ambaye alikuwa amehudumu kama mbunge wa Mvita kwa miaka 10 aliahidi kwamba atatoa huduma za afya bila malipo kwa wakazi wa Mombasa na hata kupunguza karo za shule kutwa za sekondari ili kuhakikisha watoto wote wanajiunga na shule.

Miaka mitatu baadaye, mipango hiyo inaendelea kushuhudia misukosuko.

Katika mkutano wa elimu Changamwe, wazazi walieleza changamoto wanazokumbana nazo zinazofanya wanafunzi wengi kusalia nyumbani baada ya kurejeshwa nyumbani kwa sababu ya karo.

Wazazi walisema licha ya Gavana Nassir kuanza mpango wa chakula shuleni ili kupunguza gharama ya karo ya shule za upili, wanafunzi bado wanakaa nyumbani kwa sababu ya kukosa karo.

Wazazi walisema bado wanalipa Sh12,000 kwa mwaka, lakini kulingana na Gavana Nassir mpango wake ulikuwa ni kupunguza ada hiyo hadi Sh1,500.

Gavana alisema alitia mkataba na serikali kuu akiwemo Rais William Ruto, Mwanasheria Mkuu Bi Dorcas Oduor na Waziri wa Elimu Bw Julius Ogamba kuhusu kupunguza ada za karo ya shule.

“Tumekuwa tukilalamika kila mara kuhusu ada za shule. Kwa nini watoto wetu wanatozwa ada ya juu ilhali kuna basari ambayo imepunguza gharama? Watoto wanarejeshwa nyumbanihata watahiniwa wa kidato cha nne sababu ya karo. Sijui kati ya Gavana Nassir na walimu wakuu nani anasema ukweli,” alisema Bi Elizabeth Wasai, mzazi Changamwe.

Wanafunzi wote wa chekechea na shule za sekondari hupewa chakula cha bure shuleni katika Kaunti ya Mombasa.

“Walimu wakuu waliniambia karo inayotozwa wanafunzi hutumika kutatua mishahara ya walimu wa BoM. Ili kupunguza ada kwa wazazi nilikutana na wabunge wa Mombasa ili tujumuishe basari zetu tupunguzie wazazi gharama hasa katika upande wa lishe. Nasikitia kugundua kwamba wazazi bado wanatozwa Sh12,000 na hakuna karo iliyopungua,” alisema Bw Nassir.

Katika sekta ya afya, Bw Nassir amekuwa mstari wa mbele kusajili wakazi wa Mombasa kwenye SHA, mbali na mpango wa matibabu ya bure kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano katika hospitali za umma.

Lakini wazazi walisema bado wanatozwa ada za matibabu.

Bw Nassir pia alilaumu hospitali za umma ambazo zinawalazimisha wagonjwa kulipia vipimo na dawa nje ya hospitali licha ya serikali yake kugharamia malipo kupitia bima ya afya ya umma ya SHA.

“Ni dhuluma. Tumetenga fedha kulipa usajili wa SHA kwa wagonjwa wetu lakini bado wanatumwa kufanya vipimo nje ya hospitali zetu. Hii si sawa kimaadili,” alisema.

Kulingana naye, vikwazo hivyo vinasababishwa na watu wanaohujumu utawala wake na alionya kwamba serikali yake itaanza kuwasimamisha kazi wahusika.

“Nitafanya mabadiliko makubwa katika sekta za elimu na afya. Nitawasimamisha kazi wale ambao wananihujumu. Si nilichaguliwa na wananchi? Si hizo fedha ni za wananchi? Nitapigana kwa ajili yao. Wanaohujumu miradi yangu watakiona,” alionya Bw Nassir.

Bw Nassir ameahidi kutembelea kila eneo bunge, kufanya mikutano na wazazi na kutembelea shule za upili ili kuhakikisha maagizo yake yanatekelezwa.