Habari za Kitaifa

Dawa za mamilioni ya pesa zaharibika Kemsa wagonjwa nchini wakiteseka

Na ANGELA OKETCH June 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RIPOTI ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali imefichua jinsi dawa za kuokoa maisha za thamani ya mamilioni zilivyoharibikia katika mabohari ya Mamlaka ya Usambazaji Vifaa vya Matibabu Nchini (Kemsa) huku maelfu ya Wakenya wakikosa matibabu katika hospitali za umma au kulazimika kununua dawa kwa gharama zao.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya mwaka wa kifedha uliomalizika Juni 30, 2025, dawa na vifaa vya afya vyenye thamani ya Sh376.8 milioni viliharibika vikiwa chini ya usimamizi wa Kemsa.

Miongoni mwa dawa hizo zilikuwa za Wizara ya Afya zenye thamani ya Sh23.96 milioni, zikiwemo dawa za kutibu saratani za thamani ya Sh9.26 milioni.

Hali hiyo imezua hasira kutoka kwa mashirika yanayowakilisha wagonjwa wa saratani, HIV na magonjwa sugu, yakisema ni jambo la kusikitisha wakati wagonjwa wengi wanashindwa kupata matibabu.

Mashirika hayo, yakiwemo Kenyan Network of Cancer Organisations (KENCO), Health NGOs Network (HENNET), NCD Alliance Kenya na Kenya Mended Hearts Patients Association, yalisema ripoti hiyo inaonyesha udhaifu mkubwa katika usimamizi wa dawa na mfumo wa ugavi.

“Taarifa hizi zinaonyesha hasara kubwa ya dawa, udhibiti hafifu wa mabohari na changamoto zinazowazuia wagonjwa kupata matibabu muhimu wakati wanayahitaji,” yalisema katika taarifa ya pamoja.

Ripoti hiyo pia ilibaini kuwa Kemsa ilipokea dawa za thamani ya Sh558.6 milioni zikiwa zimesalia na chini ya asilimia 75 ya muda wake wa matumizi, huku nyingine za thamani ya Sh283.9 milioni zikisambazwa kwa hospitali zikiwa zimesalia na chini ya miezi sita kabla ya kuharibika.

Mashirika hayo yamehoji jinsi dawa hizo zilivyoharibika ilhali wagonjwa wengi walikuwa wakiripoti ukosefu wa dawa katika vituo vya afya.

“Kwa nini dawa za kuokoa maisha ziliharibika kwenye mabohari huku wagonjwa wakikatiziwa matibabu au kulazimika kununua dawa kwa fedha zao?” yalihoji.

Mkaguzi Mkuu pia alibaini kuwa hakukuwa na mfumo madhubuti wa kusimamia usambazaji upya, kurejesha au kuondoa dawa zilizoharibika, hali iliyozua wasiwasi kuhusu usalama wa wagonjwa na ufuatiliaji wa dawa hizo.

Kemsa, kwa upande wake, ilieleza kuwa baadhi ya dawa hizo ziliharibika kutokana na Wizara ya Afya kutotoa maelekezo ya kuzisambaza na pia kutokana na kile ilichodai kuwa mahitaji madogo kutoka vituo vya afya.

Mamlaka hiyo ilisema jukumu lake ni kununua, kuhifadhi na kusambaza dawa, huku upangaji wa mahitaji ukifanywa na Wizara ya Afya.

Hata hivyo, mashirika ya kiraia yalisema maelezo hayo yanaonyesha hitilafu kubwa katika mfumo wa kitaifa wa ugavi wa dawa na yanahitaji uchunguzi wa kina.

Yametaka Wizara ya Afya kuitisha mkutano wa dharura wa wadau wote ili kueleza jinsi dawa zilizonunuliwa ziliachwa bila kusambazwa, huku Kemsa ikitakiwa kuchapisha ukaguzi wa dawa zote zilizo katika hatari ya kuharibika na kuweka mfumo wa haraka wa kuzisambaza katika hospitali zinazozihitaji.

Aidha, Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) imetakiwa kushughulikia ucheleweshaji wa malipo kwa hospitali unaochangia ukosefu wa fedha za kununua dawa na hivyo kusababisha upungufu wa huduma.

“Dawa hununuliwa kuokoa maisha, si kuharibikia kwenye mabohari. Kila dawa inayoharibika ni fursa iliyopotea ya kuokoa mgonjwa na kuboresha afya yake,” mashirika hayo yalisema, yakitaka hatua za haraka zichukuliwe ili kuzuia hali kama hiyo kujirudia.