Mateso hospitalini wauguzi wakikaa ngumu mgomoni
HUDUMA za afya nchini zimeendelea kutatizika huku mgomo wa wauguzi ukiingia siku ya sita, hali iliyosababisha wagonjwa wengi, hasa wajawazito na watoto wachanga, kukosa huduma muhimu katika hospitali za umma.
Chama cha Madaktari wa Uzazi na Magonjwa ya Wanawake nchini (KOGS) kimetoa wito kwa serikali kutatua mgogoro huo haraka, kikionya kuwa kucheleweshwa kwa suluhu kunaongeza hatari ya vifo vinavyoweza kuzuiliwa kwa akina mama na watoto wachanga.
Rais wa chama hicho, Dkt Kireki Omanwa, amesema huduma za uzazi zimeathirika pakubwa huku wodi za wazazi na watoto wachanga zikifurika kutokana na wagonjwa kuhamishwa kutoka hospitali ambazo hazifanyi kazi.
Alionya kuwa mgomo huo unaweza kudhoofisha juhudi za serikali kufanikisha mpango unaolenga kupunguza vifo vya akina mama na watoto wachanga kufikia mwaka 2028.
Hata hivyo, hali imeanza kubadilika katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) baada ya wauguzi kurejea kazini kufuatia makubaliano kati ya uongozi wa hospitali hiyo na Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC).
Makubaliano hayo yaliongeza marupurupu ya sare kutoka Sh15,000 hadi Sh25,000 kwa mwaka, ya huduma za uuguzi kutoka Sh20,000 hadi Sh30,000, pamoja na kuboresha yale ya likizo kulingana na daraja la kazi.
Licha ya muafaka huo, wauguzi katika hospitali nyingi za kaunti bado hawajarejea kazini.
Katibu Mkuu Msaidizi wa Muungano wa Wauguzi Kenya (KNUN), Lucy Mburu, amesema mazungumzo kati ya viongozi wa chama hicho, Baraza la Magavana na maafisa wa wizara za Afya na Kazi yalikuwa yakiendelea lakini hayakuwa yamezaa matunda.
Katika Kaunti ya Isiolo, hali imezidi kuwa mbaya kwani hata madaktari wamekuwa mgomoni kwa siku 66.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Madaktari (KMPDU), Dkt Dennis Miskellah, alisema madaktari walikosa mishahara kwa miezi mitatu, huku makato ya kodi, SHA na mikopo yakikosa kuwasilishwa kwa taasisi husika.
Kaunti za Homa Bay na Siaya pia zinakabiliwa na tishio la migomo ya madaktari kutokana na migogoro ya ajira na bima ya afya.
Katika kaunti ya Homa Bay, viongozi wa wauguzi wamemtaka Gavana Gladys Wanga kutumia nafasi yake kama mwenyekiti wa Kamati ya Wafanyakazi ya Baraza la Magavana kushinikiza suluhu ya mgogoro huo.
Katika Hospitali ya Rufaa ya Kisii, wagonjwa wengi wameelekea hospitali za kibinafsi baada ya huduma nyingi kukwama.
Hospitali ya Rufaa ya Jaramogi Oginga Odinga (JOOTRH) mjini Kisumu nayo imeelemewa baada ya kupokea wagonjwa wengi kutoka kaunti jirani.
Mkurugenzi wa huduma za uuguzi Teresa Okiri alisema hospitali hiyo sasa inapokea wastani wa wagonjwa 50 mahututi kila siku, huku wodi za wazazi, watoto wachanga na dharura zikifurika.
Katika Hospitali ya Rufaa ya Kitui, mamia ya wagonjwa walionekana wakisubiri huduma bila mafanikio.
“Tunaomba serikali isikilize malalamishi ya wahudumu wa afya ili huduma zirudi kawaida,” alisema Mary Mutua, mmoja wa wagonjwa.