HabariHabari za Kitaifa

Huzuni: Aliyekuwa waziri, Konchella, 74, afariki dunia

Na RUTH MBULA June 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

ALIYEKUWA Mbunge wa Kilgoris, Gideon Konchella, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 74 baada ya kuugua kwa muda. Bw Konchella alifariki Ijumaa, Juni 12, 2026 saa kumi alasiri katika Hospitali ya Nairobi ambako alikuwa akipokea matibabu kwa takriban wiki mbili zilizopita.

Aliyekuwa mwenyekiti wa Hazina ya Maendeleo ya Maeneo Bunge (CDF) Kilgoris na sasa Spika wa Bunge la Kaunti ya Narok, Davis Dikirr, alisema marehemu alikuwa akiugua kwa muda ingawa madaktari bado hawajatangaza rasmi chanzo cha kifo chake.

Kabla ya kuingia siasani, Konchella aliwahi kuhudumu jeshini na kupanda hadi cheo cha Kanali. Mwaka 2002 alichaguliwa kuwa Mbunge wa Kilgoris kupitia chama cha NARC na akahudumu kwa miaka 20 hadi 2022 alipogombea kiti cha Seneta wa Narok bila mafanikio.

Katika utumishi wake serikalini, aliwahi kuwa Naibu Waziri wa Afya na baadaye Waziri wa Uhamiaji wakati wa utawala wa Rais mstaafu Mwai Kibaki.

Mbunge wa sasa wa Kilgoris Julius Sunkuli alimwomboleza kama kiongozi mtulivu lakini aliyekuwa na mikakati thabiti aliyesaidia maendeleo makubwa katika eneo hilo, ikiwemo kuanzishwa kwa shule za wasichana kama Kilgoris Girls, Shartuka Girls na Enosaen Girls.

Rais William Ruto alituma salamu za rambirambi akisema Konchella alitumikia wananchi wa Kilgoris na taifa kwa heshima na uadilifu kwa karibu miongo miwili. “Kenya imepoteza kiongozi wa kizazi chake. Alielewa kuwa uongozi ni dhamana ya umma na maisha yake yalipimwa kwa mchango aliotoa kwa watu wake,” alisema Rais Ruto.

Gavana wa Narok Patrick Ole Ntutu alisema marehemu atakumbukwa kwa juhudi zake za kudumisha amani, umoja na maendeleo katika eneo la Trans Mara na Kilgoris kwa ujumla.

Naye Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula alisema alikuwa mbunge mwenye hoja nzito na mtetezi shupavu wa wananchi wake. Konchella anaacha nyuma historia ya utumishi wa umma uliodumu kwa zaidi ya miongo miwili na ambao wengi wanaamini utaendelea kuwa mfano kwa vizazi vijavyo.