MAONI: Mapema sana kusherehekea au kununa kuhusu kesi ya Gachagua
MWISHO wa kesi ya kutimuliwa kwa aliyekuwa naibu rais, Geoffrey Rigathi Gachagua, uko mbali sana.
Waambie wanaosherehekea au wanaoteta na kusonya watulie kidogo, safari yenyewe ni ndefu na haitaki hasira wala jazba.
Kwamba Mahakama Kuu imeamua kuwa hatua ya Bunge la Seneti kumtimua Bw Gachagua lilikuwa sahihi, kisha Mahakama hiyo-hiyo ikasema haki zake zilikiukwa, ni hali inayomfungulia lango kubwa yeyote anayetaka kukata rufaa.
Wala usipumbazwe na matamshi ya Bw Gachagua juzi kwamba atahakikisha muungano wa upinzani unaojiandaa kuchukua serikali mwakani umepata mgombea wa urais haraka iwezekanavyo.
Wanaosherehekea uamuzi huo wa juzi wanaamini kwamba, hata Bw Gachagua akikata rufaa, muda utayoyoma upesi sana kiasi cha kesi kutokamilika kabla ya uchaguzi mkuu ujao, hivyo atazuiwa kuwania wadhifa wowote.
Wanasema hata Mahakama ya Rufaa ikifanya kazi usiku na mchana, na ifanikiwe kutoa maamuzi kabla ya uchaguzi huo, bado kuna hatua nyingine ambapo asiyeridhika anaweza kwenda hadi Mahakama ya Upeo na kuchelewesha maamuzi ya mwisho.
Huo ni mtazamo wa watu ambao hawaoni mbali.
Wanaoteta na kusonya kutokana na maamuzi hayo, na sidhani kunaye anayeteta na kusonya kumzidi Gachagua mwenyewe, wanasema jitihada za muungano wa upinzani kutwaa serikali mwakani hazitegemei yanayoendelea mahakamani kamwe.
Ni kwa sababu hii ambapo Bw Gachagua alikimbia kwenye vyombo vya habari kuwahakikishia watu kwamba mgombea urais wa upinzani atapatikana hivi karibuni, kesi ikamilike au la.
Pamoja na kwamba hiyo ni mbinu ya upinzani kuwatuliza wafuasi wake, pia ni njia nyingine ya kuukanganya muungano wa Kenya Kwanza unaotawala, kuupa matumaini ya uongo kwamba mgombea wanayetamani kuponda atajulikana karibuni, wajiandae washike tindo mikononi!
Upinzani anaoongoza Bw Gachagua unaweza kucheza na akili za Kenya Kwanza namna hii mpaka Juni mwakani, kisa na maana kutompa adui wake wa kisiasa fursa ya kutunga na kueneza propaganda dhidi ya mgombea wao.
Pia, tangazo la Bw Gachagua kwamba mgombea wa upinzani atapatikana hivi karibuni lilinuiwa kuwahakikishia wafuasi wa muungano wa upinzani kwamba yeyote kati ya vigogo wa mrengo huo anaweza kuteuliwa, si lazima awe Bw Gachagua.
Ni njia nyingine ya Bw Gachagua kuonyesha jeuri yake dhidi ya hasidi wake mkuu wa kisiasa, Rais William Ruto, kumkumbusha kuwa hata akikosa fursa zote za kutumikia nchi hii kisiasa, hawezi kurudiana naye, tena anafanya kila awezalo kuhakikisha Bw Ruto hachaguliwi tena mwakani.
– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)