Kimataifa

Mvutano ndani ya jeshi wazua hofu kubwa kwa Rais Biya aliye madarakani kwa miaka 40

Na MASHIRIKA June 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

YAOUNDE, Cameroon:

RAIS wa Cameroon, Paul Biya, ameripotiwa kuwekwa katika hali ya tahadhari ya juu baada ya kuibuka kwa mvutano na dalili za machafuko ndani ya jeshi, hali inayozidisha hofu ya kukosekana kwa utulivu katika taifa hilo la Afrika ya Kati.

Imeripotiwa kuwa, kambi za kijeshi zimekumbwa na mgogoro wa ndani unaohusishwa na malalamiko ya mishahara, mazingira duni ya kazi na tofauti za uaminifu kwa uongozi wa kisiasa.

Hali hiyo imesababisha wasiwasi kuhusu uwezekano wa mgawanyiko ndani ya vikosi vya ulinzi vinavyotegemewa kulinda utawala wa Biya, ambaye amekuwa madarakani kwa zaidi ya miaka 40.

Taarifa zinaeleza kuwa, uongozi wa kijeshi umeongeza uangalizi katika kambi mbalimbali nchini humo, huku idara za usalama zikifanya ufuatiliaji wa mawasiliano ya maafisa wa jeshi ili kuzuia uwezekano wa uasi.

Wachambuzi wa masuala ya usalama wanasema hali hiyo inatokana na changamoto za muda mrefu ndani ya jeshi la Cameroon, ambalo limehusishwa mara kwa mara na malalamiko ya upendeleo wa kisiasa na ugawanaji usio sawa wa rasilimali.

Aidha, migogoro ya ndani ya nchi, na magharibi mwa nchi, imeongeza shinikizo kwa vikosi vya usalama.

Hali hii inajiri wakati Cameroon ikiendelea kukabiliwa na misukosuko ya kisiasa, ikiwemo mvutano kuhusu urithi wa madaraka na mabadiliko ya katiba yaliyoongeza mjadala kuhusu mustakabali wa uongozi wa Biya.

Serikali ya Cameroon haijatoa taarifa rasmi kuhusu ripoti hizo, lakini duru za karibu na Ikulu zinasema Rais Biya anaendelea kupokea taarifa za kijasusi kuhusu hali ya jeshi na usalama wa taifa kwa ujumla.

Wakati huu, wachambuzi wanaonya kuwa endapo hali hiyo haitadhibitiwa haraka, inaweza kuongeza hatari ya misukosuko ya kisiasa na kudhoofisha utulivu wa taifa hilo.