Kenya yalenga soko la Ulaya kuuza asali
KENYA imeanza safari ya kuvunja kikwazo cha muda mrefu kilichokuwa kikizuia asali yake kuingia katika soko la Umoja wa Ulaya (EU), hatua inayotarajiwa kufungua mwanya mpya wa biashara na kuongeza mapato kwa maelfu ya wafugaji nyuki nchini.
Serikali, kupitia Wizara ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo, imetangaza kuwa imekamilisha maandalizi ya Mpango wa Ufuatiliaji wa Mabaki ya Kemikali (Residue Monitoring Plan) kwenye asali, ambao ni miongoni mwa masharti muhimu yanayohitajika ili bidhaa za nyuki ziruhusiwe kuuzwa katika soko la Ulaya.
Mpango huo tayari umewasilishwa kwa Tume ya Ulaya kwa ajili ya kuidhinishwa, hatua ambayo maafisa wa serikali wanaamini itafungua milango ya masoko yenye thamani kubwa barani Ulaya na kwingineko duniani.
Akizungumza Nairobi, Katibu wa Idara ya Maendeleo ya Mifugo, Jonathan Mueke, alisema serikali pia imewekeza katika vifaa vya kisasa vya maabara kupitia Taasisi ya Huduma za Mifugo (DVS) ili kuhakikisha ubora na usalama wa asali inayozalishwa nchini unaakidhi viwango vya kimataifa.
Kwa miaka mingi, Kenya imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya kushindwa kuuza asali katika nchi za EU kutokana na kutokuwepo kwa mfumo rasmi wa kufuatilia na kudhibiti mabaki ya kemikali katika bidhaa za nyuki.

“Tunafahamu kuwa ukosefu wa mpango wa ufuatiliaji wa mabaki ya kemikali umekuwa ukikwamisha usafirishaji wa asali yetu, hasa katika nchi za EU. Hili ndilo eneo ambalo tumelipa kipaumbele ili kufungua masoko ya kimataifa,” alisema Mueke.
Hatua hiyo inajiri wakati ambapo mahitaji ya asali nchini na kimataifa yanaendelea kuongezeka. Kwa sasa Kenya huzalisha takriban tani metri 19,000 za asali kwa mwaka, huku mahitaji yakizidi tani metri 43,000. Hii ina maana kuwa nchi inakabiliwa na upungufu wa zaidi ya tani 24,000, sawa na karibu asilimia 56 ya mahitaji yote.
Kulingana na Mueke, pengo hilo linaonyesha uwepo wa fursa kubwa ya uwekezaji katika sekta ya ufugaji nyuki, kuanzia uzalishaji wa asali hadi usindikaji na biashara ya bidhaa nyingine zitokanazo na nyuki kama vile nta (wax), propolis na royal jelly.
“Sekta hii ina uwezo mkubwa kuchangia ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi. Tunahitaji ushirikiano na wadau wote ili kufanikisha uwezo huo,” alisema.
Takwimu za serikali zinaonyesha kuwa zaidi ya familia 200,000 nchini hutegemea ufugaji nyuki kama chanzo cha kipato, huku karibu asilimia 80 ya asali yote ikitoka katika maeneo Ukame na Nusu-Ukame (ASAL). Maeneo hayo yamekuwa yakionekana kuwa na mazingira yanayofaa kwa ufugaji nyuki kutokana na uwepo wa mimea asilia na matumizi madogo ya kemikali za kilimo.

Mueke anasema ufugaji nyuki unaendelea kujitokeza kama biashara yenye gharama ndogo za kuanzisha lakini yenye faida kubwa, hasa kwa vijana na wanawake.
“Tunaweza kuwapa vijana na vikundi vya wanawake mizinga ya nyuki na ndani ya miezi sita waanze kupata mapato. Ni biashara yenye uwezo mkubwa kubadilisha maisha na kuongeza kipato cha jamii nyingi,” alisema.
Mbali na uzalishaji wa asali, nyuki wana mchango mkubwa katika uzalishaji wa chakula kupitia uchavushaji mtambuka wa mazao (cross pollination). Kimataifa, zaidi ya asilimia 75 ya mazao yanayozalisha matunda na mbegu hutegemea uchavushaji wa wadudu, hususan nyuki.
Kutokana na umuhimu huo, serikali imetambua sekta ya ufugaji nyuki kama moja ya maeneo yenye uwezo mkubwa kuchangia mageuzi ya kiuchumi chini ya Ajenda ya Mageuzi ya Kiuchumi ya Kenya Kwanza. Juhudi zinazoendelea ni pamoja na kutoa mafunzo kwa wafugaji, kuimarisha huduma za nyanjani na kuhamasisha ufugaji wa nyuki kwa misingi ya kibiashara.

Baadhi ya kaunti za maeneo kame, ikiwemo Turkana, zinaibuka kama vituo muhimu vya uzalishaji wa asali, huku mashirika ya maendeleo kama Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), World Food Programme (WFP) na International Trade Centre (ITC) yakisaidia kuimarisha mtandao wa thamani wa bidhaa za nyuki kupitia mafunzo, masoko na uongezaji thamani.
Hata hivyo, wadau wanaonya kuwa sekta hiyo bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo matumizi holela ya kemikali za kilimo, mabadiliko ya tabianchi, ukataji miti na uharibifu wa makazi ya nyuki.
Mueke alisema kupungua kwa idadi ya nyuki na wadudu wengine wachavushaji mtambuka kunaweza kuathiri uzalishaji wa chakula na kuhatarisha usalama wa chakula, pamoja na maisha ya mamilioni ya wananchi wanaotegemea kilimo.
“Kulinda nyuki si suala la hiari. Ni jambo la kiuchumi, kimazingira na la kimkakati kwa mustakabali wa uzalishaji wa chakula nchini,” alisema.