Habari

Wabunge wiki hii kujadili uwezekano wa kurejesha fimbo kukomesha utundu shuleni

Na SAMWEL OWINO, BARNABAS BII June 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

USIMAMIZI wa shule, hali ya bweni na mikondo ya mawasiliano kati ya walimu na wanafunzi ni miongoni mwa masuala yatakayoangaziwa na wabunge wakianza wiki hii uchunguzi kuhusu ghasia shuleni kote nchini.

Kamati ya Bunge la Kitaifa kuhusu Elimu vilevile itachunguza miundomsingi ya shule kuhusiana na viwango vya kusajili wanafunzi.

Kamati hiyo imepangiwa kukutana na Waziri wa Elimu na Inspekta Jenerali wa Polisi katika jiji kuu la Nairobi kabla ya kuanza kuzuru shule mbalimbali kudadisi.

Katika kikao chake cha maandalizi, kamati pia haikutenga kuanzisha upya kiboko shuleni kama sehemu ya juhudi za kuangazia utovu wa nidhamu.

Mbunge wa Magarini, Harrison Kombe, mwanachama wa kamati hiyo alilalamika kuwa kupiga marufuku adhabu ya kiboko shuleni imechangia utovu wa nidhamu kuongezeka.

“Watoto wetu wanapaswa kuwa na haki na hadhi maalum? Hili wazo kuwa watoto wetu hawawezi kucharazwa au kuadhibiwa hakika limewaharibu.”

“Kiboko kweli kilikuwa kinafanya kitu kwa watoto wetu, lakini leo unapata mtoto akijibizana na mzazi au mwalimu kwa jina la haki. Ndiyo, tunasonga na ulimwengu, lakini tunawaua watoto wetu,” alisema.

Adhabu ya kiboko ilipigwa marufuku Machi 2001 kupitia notisi rasmi iliyotolewa na aliyekuwa waziri wa elimu enzi hizo Kalonzo Musyoka.

Hatua yoyote ya kuirejesha itahitaji notisi mpya kutoka kwa wizara, hivyo kuifanya suala tata kisera.

Ingawa Sheria ya Elimu inampa waziri mamlaka ya kudhibiti usimamizi wa shule na mikakati ya nidhamu, Sheria ya Watoto 2001 inapiga marufuku aina yoyote ya kudhulumu watoto kimwili na kisaikolojia.

Katika udadisi wake, kamati vilevile inatafakari kudhibiti usajili wa wanafunzi kwa kila shule na kuainisa miundomsingi ya kuhakikisha shule hazisajili wanafunzi wengi kuliko inavyoweza kumudu.

Wabunge wanasema uainishaji utasaidia kuangazia ukosefu wa usawa ambapo baadhi ya shule zimesongamana huku nyingine zikibaki bila kutumika kikamilifu licha ya kuwa na nafasi.

Mbunge wa Teso Kusini, Mary Emaase, alisema ukosefu wa nidhamu miongoni mwa wanafunzi ndilo changamoto kuu linalokabili wanafunzi, akiwalaumu wazazi kwa kutelekeza majukumu yao.

Kamati vilevile ilibaini kuwa baadhi ya walimu wakuu wa shule hutilia maanani zaidi mgao wa fedha kutoka kwa serikali kuliko maslahi ya wanafunzi.

Mwenyekiti wa Kamati Julius Melly alisema Waziri wa Elimu, Julius Ogamba atatoa ripoti kuhusu utekelezaji wa mapendekezo ya jopokazi za awali kuhusu vurugu shuleni, huku Inspekta Jenerali Douglas Kanja akiangazia masuala nyeti kuhusu usalama shuleni.

“Kamati hii haitokuwa sehemu ya kwaya ya kuomboleza; tunataka suluhu kwa suala hili, na ndiposa tunafanya hima,” alisema Bw Melly.

Wakati huo vievile, Muungano wa Kitaifa wa Walimu Nchini (KNUT) umetetea walimu dhidi ya shutuma kuwa wamechangia ongezeko la ghasia za wanafunzi na mashambulizi ya uteketezaji, wakilaumu utelekezaji wa wazazi, utovu wa nidhamu na kuingiliwa kisiasa.