KOMBE LA DUNIA: Senegal kazi ngumu, naye Messi asisimua dunia
WAHAMIAJI na mashabiki wa kimataifa walisimama na Senegal kwenye kichapo cha 3-1 mikononi mwa Ufaransa kwenye mechi yao ya ufunguzi wa Kombe la Dunia 2026 mnamo Jumanne usiku.
Hii ni baada ya mashabiki wa Senegal kunyimwa viza za kuingia Amerika.
Kocha Pape Thiaw alikuwa amesema kuwa alitarajia mashabiki wa Senegal wanaoishi jijini New York wangejitokeza kuwashabikia na kwa kweli walifanya hivyo.
“Napiga kelele na natumai kuwa wachezaji wanaweza kunisikiza uwanjani. Kama nchi mwenyeji, inasikitisha sana kuona jinsi serikali yetu inawadhalilisha raia wa mataifa mengine,” akasema Shabiki Jessica Ambres, raia wa Amerika ambaye alivalia jezi ya Senegal.
Amerika imezima mashabiki wa mataifa 39 yanayoshiriki kombe la dunia kuingia humo ikiwemo Iran, Haiti, Cote d’Ivoire na Senegal.
Kuna idadi ya juu ya raia wa Haiti na Iran Amerika ile wale wa Senegal na Cote dIvoire ni wachache.
Baada ya kipindi cha kwanza bila magoli, Ufaransa ilirejea kipindi cha pili kwa mori na kuyapata mabao yake kupitia Kylian Mbappe alifunga mabao mawili huku nguvu mpya Bradly Barcola ambaye aliingia nafasi ya Ousmane Dembele akifunga bao jingine.
Senegal walipata bao lao kupitia fataki ya nguvu mpya Ibrahim Mbaye, 18. Matokeo hayo yana maana kuwa Senegal lazima ishinde mechi zake mbili zilizosalia ili kuwa na nafasi ya kutinga raundi ya 32.
Lionel Messi naye alifunga mabao matatu mabingwa watetezi Argentina walipowakalifisha Algeria 3-0 katika Kundi J mnamo Jumatano asubuhi.
Messi, 38, sasa ni mchezaji mkongwe zaidi kufunga kwenye Kombe la Dunia na bao hilo limekuja miaka 20 baada ya kuchezea Argentina kwa mara ya kwanza katika mashindano ya 2006.
“Hii haielezeki na hakuna maneno ya kuyaeleza. Najua kuwa iwapo kuna mtu alifikiria kuwa timu hii ni bora kuliko Leo basi alinoa kwa sababu umuhimu wake ni dhahiri kwetu,” akasema Mac Allister.
Argentina itacheza dhidi ya Austria mnamo Jumatatu kule Arlington, Texas nao Algeria wavaane na Jordan siku hiyo Santa Clara, California.
Katika mechi nyingine, Austria ilipiga Jordan 3-1 kupitia mabao ya Marko Arnautovic, Romano Schimid na bao la kujifunga la Yazan Al Arab. Jordan walipata bao lao kupitia Ali Olwan.