Akili MaliMakala

Aliyekuwa mhudumu wa benki anavyoigeuza nazi za Pwani kuwa ajira na utajiri

Na SAMMY WAWERU June 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIKA ukanda wa Pwani unaojumuisha Kaunti za Kilifi, Kwale, Mombasa, Lamu, Tana River na Taita-Taveta, nazi zimeendelea kuwa zaidi ya zao la kitamaduni. Ni chakula, chanzo cha mapato na sehemu ya utambulisho wa jamii za pwani.

Hata hivyo, biashara moja inayoongozwa na mwanamke imeanza kubadili mtazamo huo, ikithibitisha kuwa nazi zinaweza kuwa injini ya ajira na fursa mpya za kiuchumi, hasa kwa wanawake katika Uchumi Samawati unaokua nchini Kenya.

Kupitia kampuni ya Nala Foods Africa Limited, mwanzilishi wake Subira Zingizi anachakata nazi kuwa bidhaa zenye thamani zaidi kama mafuta ya kupikia na ya vipodozi, pamoja na biskuti za nazi, hatua inayosaidia kuongeza mapato na kuimarisha ushiriki wa wanawake kwenye mtandao wa uongezaji thamani katika kilimo.

Akiwa na umri wa miaka 37, Subira anasema safari yake ya ujasiriamali ilianza baada ya kufanya kazi katika sekta ya benki kwa zaidi ya miaka 10. Akiwa Shahada ya Biashara kutoka Chuo Kikuu cha Kenyatta (KU), aliamua kuacha kazi ya ofisi na kuingilia biashara ya kuchakata mazao ya kilimo.

Kwa sasa, akiwa na mwanzilishi mwenza na mkurugenzi mwenza Ali Salim Mbongi, wanaendesha kampuni inayojituma kuboresha kilimo cha nazi Pwani.

“Tuliona pengo kubwa sokoni. Ingawa nazi hulimwa kwa wingi Pwani, bidhaa nyingi zinazouzwa madukani hazitoki Mombasa au Kwale,” Subira anasema.

Nazi zilizokunwa kwenye katika kampuni ya Nala Foods Africa. Picha|Sammy Waweru

Alianza biashara hiyo mwaka 2019 kwa mtindo usio rasmi, akinunua mafuta ya nazi kutoka kwa wanawake wa vijijini, kuyapakia upya na kuyauza kwa wateja. Wanawake hao, anasema, walikuwa na ujuzi wa jadi kuchakata nazi lakini walikosa masoko yenye ushindani mkuu na teknolojia ya kisasa ya uzalishaji.

Mwaka 2022, biashara hiyo ilisajiliwa rasmi baada ya kupata ufadhili wa Sh50,000 kupitia mpango wa Youth Empowerment Product Initiative, fedha zilizotumika kusajili kampuni na kuingiza bidhaa sokoni.

Katika hatua za mwanzo, uzalishaji ulikuwa wa mikono kabisa. “Wafanyakazi walikuwa wakikuna nazi kwa mikono, kuzikausha kwa kutegemea jua na kukamua mafuta bila mashine,” anasema, akieleza jinsi uzalishaji ulivyokuwa mgumu, wa gharama ya juu na wa polepole.

Mabadiliko makubwa yalijiri baada ya kampuni hiyo kunufaika na mpango wa Investing in Women in the Blue Economy – Kenya, unaotekelezwa na Africa Enterprise Challenge Fund (AECF) kwa ushirikiano na Global Affairs Canada. Kupitia mpango huo, Nala Foods ilinunua mashine za kukama mafuta, kikaushio cha nishati ya jua na vifaa vingine vya kisasa vya uzalishaji.

Subira anasema msaada huo uliibadilisha kampuni kutoka uzalishaji wa mikono hadi mfumo wa nusu-otomatiki. “Awali tulizalisha kati ya lita 20 na 50 kwa mwezi, lakini sasa tunazalisha angalau lita 200 kila mwezi,” anasema.

Aidha, kampuni hiyo kwa sasa inaajiri wanawake kati ya 12 na 15 katika nyakati za uzalishaji, wakihusika na kukuna nazi, kukausha, kuchakata na kupakia bidhaa. Hali kadhalika, hununua nazi kutoka kwa wakulima na wasambazaji kutoka Kwale na maeneo jirani, hivyo kuimarisha uchumi wa ndani kwa ndani.

Vipodozi vilivyoundwa na Subira Zingizi kupitia Nala Foods Africa Limited. Picha|Sammy Waweru

Mbali na mafuta ya nazi, Nala Foods Africa Limited pia hutengeneza bidhaa za kujipodoa na biskuti za nazi, huku ikipanga kupanua zaidi uzalishaji wa vyakula na vitafunwa vinavyotokana na nazi.

Kampuni hiyo pia imeanza kupenya masoko ya nje, Tanzania ikiwa mojawapo ya wanunuzi wake wakuu. Kwa sasa, takriban asilimia 20 ya uzalishaji wake huuzwa nje ya nchi.

Subira anadokeza kwamba ongezeko la mahitaji linachochewa na mwenendo wa watu kukumbatia bidhaa asilia na lishe bora.

Kulingana na mjasiriamali huyo, kuongeza thamani ya mazao ya shambani ndiyo njia muhimu kuhakikisha kilimo kinakuwa chanzo endelevu cha ajira na utajiri katika jamii za Pwani.