Habari za Kitaifa

Wabunge wapuuza mapendekezo ya kupunguza ushuru wa PAYE

Na DAVID MWERE June 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WABUNGE wamepuuza mapendekezo ya wataalamu wa sekta ya fedha kupunguza kiwango cha juu cha ushuru wa mapato (PAYE) kutoka asilimia 35 hadi kati ya asilimia 28 na 30, licha ya shinikizo kutoka kwa wadau mbalimbali.

Badala yake, Kamati ya Fedha na Mipango ya Kitaifa ya Bunge imependekeza marekebisho kadhaa katika Mswada wa Fedha wa 2026 yatakayopunguza baadhi ya ushuru uliopendekezwa na Wizara ya Fedha.

Kamati hiyo inakadiria kuwa hatua hiyo itapunguza mapato yanayotarajiwa kutoka kwa mswada huo kutoka Sh120 bilioni hadi Sh98.5 bilioni, hali ambayo inaweza kulazimu serikali kukopa zaidi kufadhili bajeti ya Sh4.82 trilioni ya mwaka wa kifedha wa 2026/2027.

Wakati wa zoezi la kutafuta maoni ya umma, Taasisi ya Wahasibu wa Umma Kenya (ICPAK), Chama cha Wenye Benki Kenya (KBA) na kampuni ya Deloitte walipendekeza wafanyakazi wanaopata chini ya Sh30,000 kwa mwezi wasitozwe PAYE.