Habari za Kitaifa

Ghasia za wanafunzi shuleni zapungua na kupisha lawama kuzagaa kote

Na MERCY SIMIYU June 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WIMBI la ghasia zilizoshuhudiwa hivi karibuni katika shule mbalimbali za upili nchini linaonekana kupungua, lakini sasa mjadala mkali umeibuka kuhusu nani anayefaa kulaumiwa kwa vurugu hizo zilizotatiza masomo, kuharibu mali na hata kusababisha vifo.

Wazazi, walimu, wasimamizi wa shule na maafisa wa serikali wamekuwa wakirushiana lawama huku kila upande ukijaribu kueleza chanzo cha fujo hizo.

Rais William Ruto amejiunga na mjadala huo akisisitiza kuwa jamii haipaswi kuwalaumu walimu na taasisi za serikali pekee kila mara wanafunzi wanapojihusisha na vitendo vya uharibifu.

“Watoto wetu si jukumu la serikali pekee. Kwanza kabisa ni jukumu la wazazi. Jamii inapaswa kuacha kuwalaumu walimu na taasisi za serikali kila mara wanafunzi wanapojihusisha na tabia za uharibifu,” alisema Rais Ruto alipohudhuria hafla ya Rhino Charge eneo la Wamba, Kaunti ya Samburu.

Kauli yake inajiri huku Wizara ya Elimu ikiwa bado haijateua jopo maalum aliloahidi Waziri wa Elimu Julius Ogamba kuchunguza chanzo cha ghasia hizo na kupendekeza suluhu za muda mrefu.

Hata hivyo, Chama cha Kitaifa cha Wazazi kimeelekeza lawama kwa shule na wasimamizi wa elimu, kikisema kanuni nyingi za usalama shuleni ziko katika nyaraka pekee wala hazitekelezwi kikamilifu.
Mwenyekiti wa chama hicho, Silas Obuhatsa, alisema serikali inapaswa kuhakikisha shule zote zinatekeleza masharti ya usalama kama ilivyoagizwa.

“Kama kanuni za usalama zingekuwa zinatekelezwa kikamilifu, tusingeshuhudia baadhi ya matukio haya,” alisema.

Bw Obuhatsa pia alilalamika kuwa wazazi wametengwa katika masuala yanayohusu shule na ustawi wa watoto wao.

“Wazazi ni wadau muhimu lakini hawashirikishwi vya kutosha. Wanapotengwa, matatizo mengi hayagunduliwi mapema hadi yanapogeuka migogoro mikubwa,” alisema.

Alitaja vizuizi vinavyowekwa shuleni kama moja ya changamoto kuu. Kwa mujibu wake, wazazi wengi hawawezi kuwasiliana kwa urahisi na walimu au wasimamizi wa shule kuhusu masuala yanayowahusu watoto wao.

“Leo hii kuna maeneo mengi shuleni yaliyoandikwa ‘Wafanyakazi Pekee’ na wazazi hawaruhusiwi kuingia. Hii imewafanya wazazi kujihisi wametengwa,” alisema.

Kwa upande wao, viongozi wa vyama vya walimu wanasema ghasia hizo ni kielelezo cha hali ilivyo katika jamii kwa ujumla.

Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu wa Shule za Upili na Vyuo (KUPPET), Moses Nthurima, alisema matukio ya vurugu shuleni yanaakisi yanayoonekana katika jamii.

“Tunachoona shuleni ni sawa na kinachoendelea nje. Mitaani watu wanachoma tairi, wanaharibu mali na kushiriki vitendo vya vurugu. Mvutano huo unaingia pia katika shule,” alisema.

Bw Nthurima alipendekeza shule zifungwe mapema kwa likizo ya katikati ya muhula ili kupunguza msongo wa mawazo miongoni mwa wanafunzi.