Maseneta washangaa jinsi jengo la Sh820m alilojenga Wanga linafaidi wakazi Homa Bay
MASENETA wameibua wasiwasi kuhusu matumizi ya fedha za umma katika mradi wa ujenzi wa makao makuu mapya ya Serikali ya Kaunti ya Homa Bay baada ya Gavana Gladys Wanga kushindwa kueleza kwa kina kiasi halisi kilichotumika katika ujenzi huo.
Maseneta walitaka kujua iwapo wakazi wa Homa Bay wanapata thamani ya fedha zao kutokana na mradi huo uliogharimu mamilioni.
Baadhi ya maseneta walimlaumu gavana huyo kwa kutofuata taratibu za kisheria wakati alipoanzisha mradi wa kujenga ofisi hizo mpya katika eneo la Arujo miaka miwili iliyopita.
Hata hivyo, walimsifu kwa kukamilisha mradi huo kwa muda mfupi ikilinganishwa na kaunti nyingine ambazo miradi kama hiyo imekwama kwa miaka mingi.
Makao makuu hayo mapya yalianza kujengwa Mei 2024 baada ya serikali ya kaunti kukubaliana na Shirika la Pensheni za Kaunti (CPF), ambalo lilifadhili ujenzi huo.
Rais William Ruto alizindua jengo hilo Agosti 2025 wakati wa Kongamano la Tisa la Ugatuzi lililofanyika Homa Bay.
Bi Wanga alifika mbele ya Kamati ya Seneti ya Hesabu za Umma inayoongozwa na Seneta wa Homa Bay, Bw Moses Kajwang’, kujibu hoja zilizotokana na ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka wa kifedha wa 2024/2025.
Kwa mujibu wa Mkaguzi Mkuu, Bi Nancy Gathungu, Serikali ya Kaunti ya Homa Bay inapaswa kulipa CPF jumla ya Sh820 milioni ndani ya kipindi cha miaka minne kwa mradi huo.
Maseneta walitaka kujua gharama halisi ya ujenzi, lakini gavana hakutoa maelezo hayo. Badala yake, alisema tu kwamba serikali yake italipa CPF kiasi hicho cha Sh820 milioni kama gharama ya mradi.
Alikanusha madai kuwa fedha hizo ni mkopo, akisema ni malipo ya huduma zilizotolewa na CPF kupitia fedha za pensheni za wafanyakazi wa kaunti.
Karani wa Kaunti, Profesa Bernard Muok, alisema serikali ilitambua mahitaji ya ofisi mbalimbali kabla ya kutangaza zabuni ya ujenzi.
Mkuu wa kitengo cha ununuzi, Bw Peter Odiango, alisema zabuni ya wazi ilitangazwa na kampuni tano zilionyesha nia ya kushiriki, lakini CPF pekee ndiyo iliyowasilisha zabuni ya mwisho.
Bw Odiango alisema CPF awali ilipendekeza kujenga jengo hilo kwa Sh900 milioni kabla ya kiwango hicho kupunguzwa hadi Sh820 milioni.
Hata hivyo, alikiri kuwa serikali haikuwa na makadirio rasmi ya gharama za ujenzi na ilitoa tu maelezo ya kile ilichotaka kujengwa.
Wakati huo huo, Gavana Wanga alitakiwa kueleza matumizi ya Sh500,000 kujenga choo cha mashimo chenye milango miwili katika ufuo wa Ngeri, eneo la Kaksingri Magharibi.
Alisema kiasi hicho ni cha kawaida kwa mradi wa aina hiyo, akieleza kuwa gharama hutegemea aina ya udongo wa eneo husika.
Kulingana naye, baadhi ya maeneo yanaweza kugharimu karibu Sh460,000 huku mengine yakihitaji zaidi kutokana na hali ya ardhi.
Maseneta sasa wanataka maelezo zaidi kuhusu mchakato mzima wa mradi huo ili kubaini ikiwa fedha za walipa ushuru zilitumika kwa uwazi na kwa manufaa ya wakazi wa Homa Bay.