Habari za Kaunti

Seneta lawamani kwa kusahau ‘waliomsaidia’

Na WINNIE ATIENO June 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BAADHI ya wajumbe wa Chama cha ODM akiwemo Katibu wa ODM Voi, Bw Hassan Mwaniki, wamemlaumu Seneta Jonnes Mwaruma wakidai amewatenga licha ya kumsaidia uchaguzini, akilenga kuwania ugavana 2027.

Hayo yalijiri huku wafuasi wa Chama cha ODM katika kaunti hiyo wakianza juhudi za kukipigia debe baada ya kupoteza viti vyote isipokuwa useneta na madiwani watano katika uchaguzi uliopita.

Hata hivyo, Bw Mwaruma, aliwataka viongozi wa ODM kushirikiana na kuacha migogoro.

Aliwahakikishia wajumbe kwamba chama kitaunda kamati ya uwiano ili kuwapatanisha mahasimu, na kujenga mshikamano ndani ya chama.