Siasa

Viongozi Homa Bay waahidi kusitisha uhasama na kumtafutia Ruto Tutam

Na GEORGE ODIWUOR June 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIONGOZI wa ODM kutoka Kaunti ya Homa Bay ambao walikuwa na uhasama wameahidi kuungana ili kupiga jeki juhudi za kumtafutia Rais William Ruto kura eneo hilo.

Waziri wa Fedha John Mbadi aliongoza himizo la kuwataka wanasiasa hao waungane akisema binafsi hataunga mwanasiasa mwenye uhasama na anayegawanya jamii.

“Kati ya mambo ambayo yanasababisha kaunti zetu kusalia nyuma kimaendeleo ni malumbano ya mara kwa mara. Kumekuwa na tofauti za kibinafsi, na tumeketi chini kusuluhisha kila kitu na kuamua kufanya kazi pamoja,” akasema Bw Mbadi.

Viongozi ambao wamekuwa na mgogoro ni Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga na Katibu katika Wizara ya Usalama Raymond Omollo.

Wafuasi wao wamekuwa wakikabiliana kuhusu miradi huku baadhi wakidai Bi Wanga anadandia miradi ya serikali ya kitaifa.

Bw Mbadi alikuwa akiongea katika kanisa la Kiadventista la Sombro, Kochia, eneobunge la Rangwe, Kaunti ya Homa Bay, mnamo Jumapili.

Aliwaita Bi Wanga, Dkt Omollo, Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi, Mbunge Mwakilishi wa Kike Homa Bay Joyce Osogo na Seneta wa Homa Bay Moses Kajwang’ jukwaani kisha wakashikana mikono kudhihirisha umoja wao.

Kiongozi wa Wachache Bungeni Junet Mohamed, wabunge Opondo Kaluma (Homa Bay Mjini), Boyd Were (Kasipul), Lililan Gogo (Rangwe) na Eve Obara (Kabondo Kasipul) pia walihudhuria hafla hiyo.

Viongozi wote walishikana mkono ishara kuwa wanaunga mkono chama cha ODM na serikali ya sasa kusalia uongozini mnamo 2027.

Waliahidi kuhakikisha Rais William Ruto anapata kura zote za eneo la Nyanza huku wakisisitiza kwamba marehemu Raila Odinga aliwaacha ndani ya Serikali Jumuishi.

Bi Wanga aliomba viongozi wenzake waungane pamoja kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Pia alitaka wafuasi wao wawaige ili eneo la Nyanza lisalie na umoja.

“Tumeamua kufanya kazi pamoja. Hakutakuwa na maendeleo iwapo viongozi wataendelea kulumbana,” alisema mwenyekiti huyo wa ODM.

Akaongeza: “Sasa tunajua mahali ambapo tunaenda na kile ambacho serikali imetekeleza. Utawala wa sasa utafanya nchi kupiga hatua zaidi kimaendeleo.”

Dr Omollo aliahidi kuendelea kufanya kazi na viongozi wote wa Homa Bay kuhakikisha kaunti inanawiri.

Kuhusu maadhimisho ya maandamano ya Gen-Z siki ya Alhamisi, katibu huyo wa usalama alisema serikali italinda mali ya raia, na kuhimiza watakaoshiriki kufuata sheria.

Bw Wandayi alisema viongozi wote wa Nyanza sasa wameanza kutembea pamoja, huku akisisitiza nia yao ni kuhakikisha viongozi wananufaikia miradi ya maendeleo.

“Kupitia mwongozo wa Rais Ruto na Oburu Oginga, tutatembea pamoja. Rais amedhihirisha kuwa eneo la Nyanza pia linastahili kupokea miradi ya maendeleo na anastahili kuchaguliwa kwa muhula wa pili,” akasema Bw Wandayi.