Kimataifa

Zambia yasalimu amri, rais wao wa zamani Edgar Lungu atazikwa Afrika Kusini

Na REUTERS June 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JOHANNESBURG, Afrika Kusini:

MAHAKAMA ya Rufaa ya Afrika Kusini Jumatano iliamua kwamba familia ya aliyekuwa Rais wa Zambia, Edgar Lungu, ndiyo yenye haki ya kuamua mahali atakapozikwa.

Uamuzi huo ulibatilisha uamuzi wa Mahakama Kuu uliokuwa umeipa serikali ya Zambia ruhusa ya kuurejesha mwili wa kiongozi huyo wa zamani nchini humo na kuandaa mazishi ya kitaifa.

Lungu, ambaye aliiongoza Zambia kuanzia 2015 hadi 2021, alifariki akiwa Afrika Kusini mnamo 2025. Aliaga dunia akipokea matibabu katika hospitali moja nchini humo.

Mwili wake umekuwa ukihifadhiwa Afrika Kusini tangu wakati huo huku familia yake na serikali ya Zambia zikivutana kuhusu mahali ambapo mazishi yake yanafaa kuandaliwa na pia atakavyozikwa.

Serikali ilitaka azikwe katika eneo maalumu la kuzikwa marais wa zamani jijini Lusaka huku familia yake nayo ikiamua azikwe katika eneo teule Afrika Kusini.

Lungu na mrithi wake, Rais wa sasa Hakainde Hichilema, walikuwa na uhasama mkali kisiasa wakizozania uongozi wa taifa hilo.

Familia ya Lungu imesema kuwa marehemu aliweka wazi kuwa Rais Hichilema hafai kuruhusiwa kuhudhuria mazishi yake na lazima watimize matakwa yake.

Mwanasheria Mkuu wa Zambia, Mulilo Kabesha, aliambia Reuters kwamba serikali inaheshimu uamuzi wa Mahakama ya Rufaa ya Afrika Kusini ingawa haikubaliani na uamuzi huo.

Kwa hivyo, hawatakata rufaa na wataacha familia ya kiongozi huyo imzike Afrika Kusini.

“Tuna haki ya kukata rufaa lakini hatutafanya hivyo kwa sababu tunataka suala hili liishe na rais wa zamani azikwe,” akasema Kabesha.

Kwenye uamuzi wake, Mahakama ya Rufaa ya Afrika Kusini ilisema serikali ya Zambia imeshindwa kuthibitisha kuwa ina haki ya kisheria kupuuza matakwa ya familia kuhusu mahali na namna Lungu anavyopaswa kuzikwa.

Mahakama pia ilikataa hoja ya Zambia kwamba kulikuwa na makubaliano ya mwisho na familia kuhusu mazishi hayo.

Ilisema ushahidi ulionyesha kuwa mazungumzo yalikuwa bado yanaendelea na kwamba hakukuwa na makubaliano ya mwisho.

Serikali ya Afrika Kusini imesema ina wajibu wa kuheshimu matakwa ya familia ya Lungu, lakini pia inaamini kuwa mazishi ya kitaifa Zambia yangekuwa njia bora zaidi ya kumuenzi kiongozi huyo wa zamani.

Kwa miaka sita ambayo alikuwa madarakani, Lungu aliizamisha Zambia katika lindi kubwa la madeni.

Mnamo 2020, nchi hiyo ilishindwa kulipa madeni yake kwa mashirika ya kimataifa ya kifedha na ni kati ya masuala yaliyochangia kushindwa kwake uchaguzini.

Rais Hichilema naye anatarajiwa kuwania muhula wa pili wa miaka mitano katika uchaguzi utakaofanyika Agosti mwaka huu.