Habari za Kitaifa

IEBC yafichua ratiba ya kura za mwaka ujao, na tarehe ya maafisa wa umma kujiuzulu

Na NDUBI MOTURI June 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MAAFISA wa umma wanaonuia kuwania nyadhifa mbalimbali katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027 sasa wamesalia na chini ya siku 230 kujiuzulu baada ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuzindua rasmi ratiba ya maandalizi ya uchaguzi huo.

Ratiba hiyo, iliyozinduliwa Jumatano katika jumba la KICC jijini Nairobi, imeweka tarehe muhimu kwa vyama vya kisiasa, wagombeaji binafsi, maafisa wa umma na wadau wengine wa uchaguzi kuelekea kura ya Agosti 10, 2027.

Hatua hiyo inaashiria kuanza rasmi kwa maandalizi ya uchaguzi unaotarajiwa kuwa miongoni mwa chaguzi zenye ushindani mkali zaidi nchini huku vyama vya kisiasa vikianza kupanga mikakati ya kuwania urais, ugavana, ubunge na uwakilishi wa kaunti.

Miongoni mwa masharti muhimu yaliyowekwa katika ratiba hiyo ni hitaji la maafisa wa umma wanaotaka kugombea nyadhifa za kisiasa kujiuzulu angalau miezi sita kabla ya uchaguzi mkuu.

Hii ina maana kwamba maelfu ya maafisa wa serikali wanaotaka kuingia kwenye siasa sasa wana muda mfupi wa kufanya maamuzi kuhusu mustakabali wao.

IEBC pia imeagiza vyama vya kisiasa kuwasilisha orodha za wanachama wao kufikia Machi 16, 2027.

Kufikia tarehe hiyo, vyama vitatakiwa pia kuwasilisha majina ya wanaotaka tiketi za uteuzi pamoja na tarehe na maeneo ya kura za mchujo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mwenyekiti wa IEBC, Erastus Ethekon, alisema tume hiyo imejitolea kuhakikisha uchaguzi wa mwaka 2027 unakuwa wa uwazi, shirikishi na unaozingatia sheria.

“Tumesikiliza maoni ya Wakenya na tutaendelea kufanya hivyo. Kuna maeneo ambayo yametajwa kuwa na changamoto na tutaendelea kuyashughulikia ili kuhakikisha uchaguzi unakuwa wa kuaminika,” alisema.

Kwa mujibu wa ratiba hiyo, vyama vya kisiasa vitatakiwa kukamilisha kura za mchujo na kutatua migogoro yote ya ndani kufikia Mei 9, 2027.

Tarehe hiyo pia ni muhimu kwa wagombeaji binafsi.

Mtu yeyote anayetaka kuwania kiti kama mgombeaji huru atalazimika kuwa ameacha uanachama wa chama chochote cha kisiasa kufikia siku hiyo.

Kamishna wa IEBC, Ann Nderitu, alisema shughuli za uteuzi wa wagombeaji wa vyama vya kisiasa na wale huru zitafanyika kati ya Mei 29 na Juni 11, 2027.

Alisema wagombeaji wote watatakiwa kuwasilisha stakabadhi zao binafsi katika vituo vitakavyotengwa na tume hiyo huku migogoro ya uteuzi ikitarajiwa kuwasilishwa kabla ya Juni 12, 2027 na kusikizwa ndani ya siku 10.

Ratiba hiyo pia inaonyesha kuwa kampeni za uchaguzi mkuu zitaanza rasmi Mei 29, 2027 na kumalizika Agosti 7, 2027.

Hata hivyo, uzinduzi wa ratiba hiyo ulikosolewa na viongozi wa muungano wa upinzani waliodai kuwa IEBC imeandaa baadhi ya mipango muhimu bila kuwashirikisha wadau wa kisiasa ipasavyo.

Aliyekuwa Mwanasheria Mkuu, Justin Muturi, aliyemwakilisha kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka pamoja na viongozi wengine wa upinzani, alisema juhudi za upinzani kushirikishwa katika maandalizi ya uchaguzi zimekuwa zikipuuzwa.

Bw Muturi alisema uchaguzi ni mali ya wananchi na kwamba mpango wa shughuli za uchaguzi haupaswi kuonekana kama hati ya ndani ya IEBC bali makubaliano ya kitaifa yanayoathiri namna uchaguzi utaendeshwa.

“Inasikitisha kuona IEBC ikizindua mpango wa uchaguzi wa mwaka 2027 bila kuonyesha kuwa imefanya mashauriano ya maana na wadau wa kidemokrasia ambao wataathiriwa na mpango huo,” alisema.

Aliongeza kuwa imani ya wananchi haiwezi kujengwa kupitia siri na kutengwa kwa wadau muhimu.

“Gharama ya mashauriano ni ndogo sana ikilinganishwa na gharama ya uchaguzi unaobishaniwa. Kenya haiwezi kumudu uchaguzi mwingine ambao uhalali wake unaanza kutiliwa shaka kabla hata ya kura kupigwa,” alisema.

Upinzani pia ulitaka Hifadhidata ya Kitaifa ya Usajili wa Watu ichunguzwe na kukaguliwa kabla ya ukaguzi wa sajili ya wapigakura kufanyika.

Kwa mujibu wa Bw Muturi, dosari zozote katika mfumo wa usajili wa wananchi zinaweza kuathiri moja kwa moja sajili ya wapigakura.

Wakati huo huo, Jaji Mkuu Martha Koome alitoa wito kwa IEBC kusimamia kwa uthabiti Kanuni za Maadili ya Uchaguzi na kuwachukulia hatua kali wanasiasa wanaochochea vurugu.

“Ikiwa mtu atakiuka kanuni za maadili ya uchaguzi, basi apigwe marufuku kushiriki uchaguzi mkuu,” alisema.

Bi Koome alionya kuhusu ongezeko la makundi ya wahuni wanaotumiwa kuzima wapinzani au kuvuruga mikutano ya kisiasa.

Alisema hali hiyo imekuwa tishio kwa demokrasia na maisha ya kawaida ya mamilioni ya Wakenya ambao hawahusiki moja kwa moja na siasa.

“Nchini kuna watu wachache sana wanaopata riziki kutokana na siasa lakini matendo yao yanaathiri maisha ya mamilioni ya Wakenya wanaojitafutia riziki kwa njia nyingine. IEBC ina mamlaka ya kuhakikisha sheria zinafuatwa na inapaswa kutumia mamlaka hayo kwa ujasiri,” alisema.

Naye Bw Ethekon alionyesha wasiwasi kuhusu tabia inayozidi kushamiri ambapo baadhi ya wanasiasa huajiri vijana kwa madai ya kulinda kura au kushinikiza wapinzani wakati wa uchaguzi.

Alisema mwenendo huo unatishia amani na uaminifu wa uchaguzi wa mwaka 2027 na kwamba tume itafanya kila iwezalo kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika kwa amani, uwazi na kwa kuzingatia sheria.