Ruto aenda kukagua ujenzi wa Bomas wakati jiji lilipofungwa kuzima maandamano
NAIROBI ilipokuwa chini ya ulinzi mkali Wakenya wakiadhimisha miaka miwili tangu maandamano ya Gen Z, Rais William Ruto alitembelea mradi unaoendelea wa ujenzi wa Bomas of Kenya na kutumia fursa hiyo kuhimiza Wakenya kukataa siasa za mgawanyiko na ukabila.
Rais Ruto aliwaonya viongozi wa kisiasa dhidi ya kutumia matamshi yanayochochea chuki, ukabila na migawanyiko ya kikanda, akisema siasa za aina hiyo zinatishia umoja wa taifa na maendeleo ya nchi.
Aliwataka wananchi kuwahukumu viongozi kwa misingi ya sera, mipango ya maendeleo na maono yao kwa taifa badala ya kuegemea ukabila au maeneo wanakotoka.
“Hatutaki kuruhusu siasa za mgawanyiko na chuki kushamiri nchini. Kila kiongozi awasilishe mipango, ajenda na maono yake kwa Kenya. Wakenya wana uwezo wa kutambua ajenda itakayoinufaisha nchi,” alisema Rais Ruto.
Wiki iliyopita, Rais alijaribu kutuliza hali ya kisiasa kabla ya maandamano ya Juni 25 kwa kukanusha madai mbalimbali kuhusu mpango wa serikali wa ushuru kwa mwaka wa kifedha unaoanza Julai 1, alipotia saini Mswada wa Fedha wa 2026 kuwa sheria.
Katika hotuba yake wakati wa kutia saini sheria hiyo, Rais alitumia muda kueleza masuala yaliyozua utata kuhusu mswada huo huku akitangaza hatua mbalimbali za kuwafaidi wananchi kupitia bajeti ya mwisho ya muhula wake wa kwanza.
Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa Rais kutia saini sheria hiyo muhimu ya ushuru kabla ya Juni 25 tangu aingie madarakani, tarehe ambayo imekuwa ikiambatana na maandamano ya umma katika miaka ya hivi majuzi.