Habari za Kitaifa

Korti yaonya mwanajeshi wa zamani kukoma kutishia familia ya mke anayedaiwa kuua

Na RICHARD MUNGUTI June 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA imeamuru afisa wa zamani wa Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF), Kapteni mstaafu Edwin Muthomi Kaunga, kusitisha mara moja madai ya vitisho, unyanyasaji na usumbufu dhidi ya familia ya mwanamke anayedaiwa kumuua.

Katika hatua ya kulinda familia ya marehemu Ann Mugweru, mahakama pia imeagiza polisi kuhakikisha kuwa Kapteni Kaunga hataendelea kutoa vitisho hivyo.

Mahakama ilimwelekeza Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Nakuru (OCS) kutekeleza amri hiyo kwa kwenda katika Gereza la Naivasha Maximum ambako Kaunga anazuiliwa na kumpatia rasmi agizo la mahakama.

Aidha, mahakama iliamuru Kaunga kuacha kumpigia simu dadake marehemu na kumtishia.

Ilielezwa pia kuwa afisa huyo wa zamani wa KDF amekuwa akitishia kumchukua mtoto wa kiume anayedai alipata na marehemu.

Amri hizo zilitolewa kufuatia ombi lililowasilishwa na Bi Serah Nyokabi Mugweru, dadake marehemu, pamoja na aliyekuwa Gavana wa Nairobi Mike Sonko.

Mahakama ilielezwa kuwa Bw Sonko amekuwa akimsaidia mtoto aliyeachwa na marehemu.

Kupitia maombi hayo, Bw Sonko aliitaka mahakama kuingilia kati na kulinda haki za familia ya marehemu pamoja na mtoto huyo.

Mahakama ya Nakuru ilitumia mamlaka yake kulinda familia hiyo ambayo ilikumbwa na msiba baada ya Bi Mugweru kudaiwa kuuawa kikatili na mumewe.

Katika amri za muda zilizotolewa Jumatano, Hakimu Mkuu Mwandamizi Vincent Adet Okello alimzuia Kaunga kuwanyanyasa, kuwatisha au kuwahangaisha wanafamilia wa marehemu.

Hatua hiyo inatokana na kesi ya mauaji iliyotikisa nchi mwezi Aprili mwaka huu, ambapo Bi Mugweru, mama wa mtoto wa miaka mitano, alidaiwa kudungwa kisu hadi kufa wakati wa mzozo wa kifamilia mjini Nakuru.

Baada ya tukio hilo, Sonko alianza kumsaidia mtoto huyo na kushiriki katika malezi yake, huku akichapisha mara kwa mara maendeleo yake kwenye mitandao ya kijamii.

Katika hati za mahakama, familia ya marehemu ilisema imeendelea kuishi kwa hofu licha ya mshukiwa kukamatwa na kuwekwa rumande.

Katika kiapo chake, Bi Nyokabi alidai kuwa Kaunga ameendelea kuwatesa wanafamilia akiwa kizuizini kupitia simu.

“Cha kushangaza ni kwamba tangu akamatwe, amekuwa akinitishia, kuninyanyasa na kunihangaisha mimi pamoja na familia yangu,” alisema.

Alidai kuwa jamaa kadhaa wamepokea simu kutoka kwa mtu anayejitambulisha kama Edwin na kutishia kuwa atamchukua mtoto aliyeachwa na marehemu.

Kutokana na madai hayo, familia iliomba mahakama iingilie kati haraka ikisema usalama na amani yao bado viko hatarini.

Mahakama pia ilimuagiza OCS wa Kituo cha Polisi cha Nakuru kusimamia utekelezaji wa amri hizo. Kesi hiyo itatajwa tena Julai 7, 2026.