WANAHARAKATI watano waliotoweka baada ya kukamatwa wakati wa maandamano ya kumbukumbu ya Gen Z ya Juni 25, walipatikana wakiwa na majeraha na sasa wanapokea matibabu katika Hospitali ya Nairobi Women’s, huku wakidai walitekwa nyara, kuteswa na baadaye kutupwa sehemu tofauti jijini Nairobi.

Waliojitokeza ni Frederick Odhiambo Ojiro, Michael Ngige almaarufu Jomo Kenyatta Junior, Muteti Mulinge, Collins Ochieng na Elijah Alam.

Hata hivyo, mwanaharakati mwingine, Davis Lichuma, hakuwa amepatikana kufikia Jumamosi alasiri, hali iliyozua hofu mpya kuhusu kutoweka kwa watu kwa lazima.Wanaharakati hao walidai walikamatwa karibu na Bunge wakati wa maandamano kabla ya kutoweka, jambo lililosababisha mashirika ya kutetea haki za kibinadamu na waandamanaji kutaka polisi waeleze waliko.

Akizungumza akiwa hospitalini, Collins Ochieng alisema mara baada ya kukamatwa waliingizwa kwa nguvu ndani ya magari aina ya Subaru, wakafungwa vitambaa usoni na kupelekwa eneo wasilolijua ambako waliteswa walipokuwa wakihojiwa.

Alidai waliokuwa wakiwahoji walikuwa wakitaka kujua ni nani aliyekuwa akifadhili maandamano hayo na walimtaja mtu aliyeitwa Hussein wakisema wangemkamata pia.

Ochieng alisema walibaki wamefungwa macho hadi saa saba usiku wa kuamkia Jumamosi walipoachiliwa na kutupwa kando ya Barabara ya Lang’ata.

Kutoka hapo walitembea hadi Kibera kabla ya kupanda pikipiki kuelekea Kanisa la All Saints, walikowasiliana na shirika la Defenders Coalition lililowasaidia kufika hospitalini.

Frederick Odhiambo Ojiro alisema walipigwa vibaya wakiwa kizuizini na kwamba hata hawezi kutembea kutokana na majeraha aliyopata.

‘Wangetufikisha mahakamani kama walidhani tumefanya kosa badala ya kututesa,’ alisema.

Mwanaharakati Njeri Mwangi alilaani madai hayo akisema ni ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu na akatoa wito kwa serikali kuheshimu Katiba na kuwajibisha wahusika.

Matukio hayo yalijiri saa chache baada ya Tume ya Haki za Kibinadamu Kenya (KHRC) kutangaza kuwa watu sita waliokuwa wametoweka baada ya maandamano hayo walikuwa wamepatikana katika maeneo tofauti ya Nairobi wakiwa na majeraha na kudai waliteswa mikononi mwa waliowakamata.

Shirika la Amnesty International Kenya limetaka Mamlaka Huru ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA) pamoja na Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu (KNCHR) kufanya uchunguzi wa haraka kuhusu madai ya mateso na kutoweka kwa lazima.

Aidha, limetaka Huduma ya Kitaifa ya Polisi kufichua mara moja aliko Davis Lichuma na kuhakikisha anaachiliwa akiwa salama, likisema kila saa inayopita bila taarifa inaongeza hofu kuhusu usalama wake.

Kufikia wakati wa kuchapishwa kwa taarifa hiyo, Huduma ya Kitaifa ya Polisi haikuwa imetoa kauli kuhusu madai hayo.