VITUKO VYA MASTAA: Kyle Walker kidume cha mbegu, ana watoto saba!
KYLE Walker na mkewe Annie Kilner wamejaliwa mtoto wao wa tano pamoja.
Marafiki walithibitisha kupitia mitandao ya kijamii kuwa mtoto huyo wa kike alizaliwa mapema wiki iliyopita huku mama pamoja na mtoto wakiendelea vizuri.
Walker ambaye ni mwanasafu wa gazeti la The Sun na beki wa zamani wa Uingereza, alikuwepo wakati wa kuzaliwa kwa kimalaika hicho.
Huyo ni binti wao wa kwanza pamoja ikizingatiwa kuwa Walker, 35, na Annie, 33, wana watoto wanne wa kiume.
Chanzo kimoja kilisema: “Walker na Annie wamepita wamefurahi sana kumkaribisha msichana mdogo katika nyumba yao ya familia. Sogora huyo hakukaa mbali na Annie kipindi chote cha kuzaliwa kwa mtoto huyo.”
Annie alithibitisha habari hiyo katika taarifa na kusema: “Mtoto wetu wa kike na wa thamani sana yuko hapa salama. Tuna upendo ambao sisi sote tunahisi na furaha ambayo tayari mtoto huyu ameleta katika familia yetu.”
Annie alithibitisha kuwa alikuwa na ujauzito wa mtoto wao wa tano mapema mwaka huu. Marafiki walisema habari hizo za furaha ziliwaleta karibu zaidi kama wanandoa.
Walker, ambaye pia ana mtoto wa kiume na wa kike na Lauryn Goodman, alitangaza kustaafu soka ya kimataifa mwezi Machi.
Aliajiriwa kuwa mwandishi wa gazeti la The Sun mwezi uliopita na alimsifu kocha Thomas Tuchel kwa mabadiliko aliyofanyia Uingereza ambao sasa watakutana na DR Congo katika hatua ya 32-bora kwenye Kombe la Dunia.
Walker ambaye ni beki wa Burnley, alichezea Uingereza mara 96 na mechi yake ya kwanza ilikuwa dhidi ya Uhispania mnamo 2011 akiwa na umri wa miaka 21 pekee.
Beki huyo alinogesha mechi 24 katika michuano mitano mikuu kuanzia Euro 2016 hadi Euro 2024.