Habari za Kitaifa

Deni la Sh27 bilioni kwa hospitali za kaunti lafichua nyufa katika mpango wa SHA

Na COLLINS OMULO June 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

HOSPITALI nchini kote zinang’ang’ana na mzigo wa malimbikizi ya madeni ambayo hayajalipwa yanayofikia takriban Sh27 bilioni, hali inayofichua nyufa kwenye mpango wa serikali wa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA).

Ripoti ya Mdhibiti wa Bajeti (CoB) inaashiria kuwa SHA ilidaiwa na vituo vya afya vya kaunti kiasi kisichopungua Sh26.87 bilioni kufikia Machi 31, 2026, karibu mara tatu ya Sh8.29 bilioni zilizodaiwa kufikia mwisho wa Disemba 2025.

Deni hilo linalozidi kuongezeka limejiri licha ya hakikisho kutoka kwa Rais William Ruto kuwa SHA inafanya kazi na vituo vya afya vinalipwa bila kuchelewa.

Mamlaka hiyo ilipozinduliwa Oktoba 2024, ilisifiwa kama mpango wa mabadiliko utakaowahakikishia Wakenya wote upatikanaji wa huduma za afya kwa bei nafuu.

Ilianzisha Hazina ya Afya ya Jamii (SHIF) iliyochukua nafasi ya Bima ya Kitaifa kuhusu Afya (NHIF) iliyovunjiliwa mbali.

Lakini ripoti ya CoB imeashiria taswira ya kutamausha kuhusu vituo vya afya vinavyoelekea kusambaratika kifedha.

Ripoti hiyo imefichua kuwa kaunti ya Nakuru imetwikwa mzigo mkubwa zaidi, kiasi cha Sh2.81 bilioni za deni linalodaiwa Hazina ya Kuboresha Huduma (FIF) zinazojumuisha Sh2.4 bilioni zinazodaiwa na SHIF na Sh432.9 milioni na NHIF.

Kakamega inafuata kwa Sh1.3 bilioni inazodai ambapo NHIF ilijumuisha Sh241.4 milioni kufikia Machi 31, 2026.

Nyeri ilidaiwa Sh632 milioni na SHIF, Mombasa Sh596.7 milioni ambapo SHIF inajumuisha Sh357.1 milioni na NHIF Sh239.6 milioni.

Kiambu ilidaiwa Sh474.8 milioni na SHIF, Garissa ilidaiwa Sh429.48 milioni na SHIF pamoja na NHIF, deni la Bomet lilikuwa Sh421.69 milioni ambapo NHIF ilijumuisha Sh54.2 milioni, Homa Bay Sh390.3 milioni na Bungoma Sh358.5 milioni.

Kajiado ilifuatia kwa Sh343.8 milioni, Kitui Sh333 milioni, Siaya Sh287.47 milioni, Kisumu Sh282.39 milioni, Elgeyo Marakwet Sh197.86 milioni, Migori Sh185.4 milioni, Nyandarua Sh183 milioni na tharaka Nithi Sh173.1 milioni.