Habari za Kitaifa

Serikali hatimaye yajipatia kitita cha Sh204 bilioni baada ya dili ya kuuza Safaricom kupita

Na DENNIS MUSAU, FATUMA BARIKI June 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI ya Kenya imevuna Sh204.3 bilioni baada ya dili ya kuuza hisa zake katika Safaricom iliyokuwa inapingwa mahakamani hatimaye kukamilika.

Serikali, kupitia Wizara ya Fedha iliuzia kampuni ya Vodacom ya Afrika Kusini asilimia 20 ya hisa mnamo Desemba 2025 katika dili iliyoibua pingamizi kutoka kwa pande tofauti tofauti.

Nyingi ya pingamizi zilihusu bei ambayo Serikali iliuza hisa hizo, wadau wakisema ilikuwa chini mno ikilinganishwa na thamani ya kampuni hiyo.

Miongoni mwa sauti kuu zilizokuwa zinapinga ni Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro huku makundi mengine ya wanaharakati yakielekea mahakamani.

Waziri wa Fedha John Mbadi, hata hivyo, alitetea vikali uuzaji huo, akisema ilikuwa bei sawa na kwamba serikali itanufaika kwa kupata fedha za kukithi mahitaji mengi ya kuendesha nchi.

Kwa kujipatia hisa hizo, ina maana sasa Vodacom itakuwa na usemi mkubwa zaidi katika operesheni za kampuni hiyo kwa kuongeza hisa zake hadi kufikia asilimia 55. Serikali ya Kenya sasa imesalia na asilimia 15.

Kesi ya kupinga kuuzwa huko imekuwa ikiendelea mahakamani mpaka majuzi ambapo Mahakama ya Rufaa ilipoitupilia mbali na kufungua mlango kwa uuzaji huo kukamilishwa.