Habari

Mashabiki wa soka Mlolongo walia kuvamiwa na magenge usiku

Na STANLEY NGOTHO July 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MASHABIKI wa soka wanaotoka kutazama mechi za Kombe la Dunia usiku Mlolongo wameelezea hofu kufuatia ongezeko la mashambulizi ya magenge ya wahalifu wanaotumia panga kuwashambulia.

George Sabario Motanya, mwenye umri wa miaka 38, alisema alivamiwa usiku wa Juni 12 alipokuwa akitoka kutazama mechi ya Kombe la Dunia kati ya Canada na Bosnia na Herzegovina.

Alisema alishambuliwa na watu wanne akisubiri kufunguliwa lango la nyumba yake.

“Walinikata kwa mapanga na kuniacha nikivuja damu. Nilipoteza meno saba na hadi sasa sijarejea kutazama mechi za Kombe la Dunia. Nahitaji Sh71,000 ili kupandikizwa meno mapya,” alisema.

Tukio hilo liliripotiwa katika Kituo cha Polisi cha Mlolongo.

Mkazi mwingine, Joe Mutuku, alisema alijeruhiwa mkononi kwa panga Juni 28 alipokuwa akitoka kutazama mechi kati ya Croatia na Ghana. Alisema aliponea chupuchupu baada ya kupiga kelele zilizowatisha washambuliaji.

Katika tukio jingine, mwanamke mwenye umri wa miaka 24 alisema alibakwa na genge hilo usiku wa Juni 27 baada ya yeye na mpenzi wake kuvamiwa walipokuwa wakirejea nyumbani. Alidai mpenzi wake alikimbia na kumwacha mikononi mwa washambuliaji waliompora mali kabla ya kumbaka.

Kwa sasa anaendelea kupokea matibabu na ushauri nasaha.

Waathiriwa walisema washambuliaji hao huwa kati ya vijana wanne hadi watano wenye mapanga na silaha nyingine, huku baadhi wakidaiwa kuvaa barakoa na hata makoti yanayofanana na yale ya polisi.

Msimamizi wa Wadi ya Mlolongo, Shedrack Mutei, alisema visa vya uhalifu vimeongezeka wakati wa Kombe la Dunia kutokana na mechi nyingi kuchezwa usiku, na kuitaka idara ya usalama kuimarisha doria.

Kamanda wa Polisi wa Athi River Magharibi, Anderson Mbae, alisema uchunguzi unaendelea na kwamba doria zimeimarishwa ili kuwakamata wahalifu hao.