Wetang’ula apanga Magharibi nyuma ya Ruto 2027
Spika wa Bunge la Kitaifa, Moses Wetang’ula, amewataka wakazi wa eneo la Magharibi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kama wapigakura ili waweze kumuunga mkono Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Akizungumza katika eneo la Kimang’eti, Kaunti Ndogo ya Malava, wakati wa hafla ya kuchangisha fedha za kununua ardhi kwa ajili ya ujenzi wa Taasisi ya Mafunzo ya Ufundi ya Kimang’eti (TTI), Wetang’ula alisema eneo la Magharibi linapaswa kumpa Rais Ruto muhula wa pili kutokana na miradi ya maendeleo ambayo serikali yake imeanzisha katika ukanda huo.
Alisema bado kuna maelfu ya watu wenye vitambulisho vya kitaifa au wanaostahili kuvipata lakini hawajajiandikisha kupiga kura.
“Tunao watu wengi wenye vitambulisho lakini hawajajiandikisha kama wapigakura. Nawahimiza wote wajitokeze kujiandikisha na mwaka ujao tumchague tena Rais William Ruto. Miradi ya maendeleo ambayo ameleta katika eneo letu inanipa ujasiri wa kuwaomba mfanye hivyo,” alisema.
Wetang’ula alitaja ujenzi wa hospitali mbili za kiwango cha sita katika kaunti za Kakamega na Bungoma kuwa miongoni mwa miradi mikubwa inayotekelezwa na serikali.
Alisema hospitali hizo zitawawezesha wakazi wa Magharibi kupata matibabu maalumu karibu na makazi yao badala ya kusafiri hadi Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Moi (MTRH) mjini Eldoret au Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) jijini Nairobi.
“Kuna hospitali mbili za kiwango cha sita zinazojengwa, moja Kakamega na nyingine Bungoma. Wananchi wetu hawatalazimika tena kwenda MTRH au KNH kutafuta matibabu maalumu,” alisema.
Spika huyo pia alifananisha safari ya kisiasa ya Rais Ruto na simulizi la Daudi katika Biblia, akisema viongozi na wananchi wa Magharibi walisimama naye wakati wa uchaguzi wa mwaka 2022 licha ya changamoto alizokuwa akipitia.
Alidai kuwa wakati huo aliyekuwa Rais, Uhuru Kenyatta, hakumuunga mkono Ruto, lakini wakazi wa Magharibi waliendelea kumuunga mkono.
“Mwaka 2022 tulisimama na Rais Ruto. Safari yake inafanana na ya Daudi katika Biblia. Kwa hivyo mwaka 2027 tusimame naye tena na tumchague kwa muhula wa pili,” alisema.
Wetang’ula pia alisema taasisi ya mafunzo ya ufundi inayopangwa kujengwa Kimang’eti itabadilisha uchumi wa eneo hilo kwa kufungua nafasi mpya za biashara na ajira kwa wakazi.
Alieleza kuwa uwepo wa taasisi hiyo utaongeza shughuli za kiuchumi kupitia biashara ndogo ndogo kama uuzaji wa mboga, saluni, huduma za bodaboda pamoja na biashara nyingine zinazoendeshwa na vijana.
Waziri wa Afya, ambaye pia alihudhuria hafla hiyo, aliunga mkono wito wa Spika huo kwa kuwahimiza wananchi wanaostahili kujiandikisha kama wapigakura kutumia zoezi linaloendelea la uandikishaji.
Aidha, alimshutumu muungano wa upinzani kwa kile alichodai ni kuendeleza siasa za ukabila na kupinga juhudi za Rais Ruto za kusambaza miradi ya maendeleo kwa usawa katika sehemu mbalimbali za nchi.
Alisema wakati wa utawala wa marais Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta hakukuwa na mijadala kuhusu rais kuhudumu muhula mmoja pekee.
“Lakini sasa kwa sababu ni Rais Ruto, kuna watu wanaodhani urais ni wa jamii moja pekee. Hata kama Rais Ruto angeondolewa, ni nani angechukua nafasi yake? Yule anayezungumzia hisa? Alipokuwa Naibu Rais alisema Waluo, Waluhya na hata Wasomali wasiwe serikalini wala wasipate maendeleo. Katika uchaguzi ujao tutawashinda kwa kura milioni tatu,” alisema Waziri huyo.
Naye Gavana wa Kakamega, Fernandes Barasa, aliwataka wakazi wa eneo hilo kuendelea kuiunga mkono serikali ya Kenya Kwanza akisema kaunti hiyo inaendelea kunufaika na miradi mbalimbali ya maendeleo na miundombinu.
Aliwahimiza wananchi kutumia kikamilifu mpango unaoendelea wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) wa kuandikisha wapigakura wapya na kuweka malengo makubwa ya kuongeza idadi ya wapigakura katika eneo lote la Magharibi.
Barasa alisema Kakamega inalenga kuwa na wapigakura milioni 1.5 waliosajiliwa, Bungoma milioni 1.2, Busia laki sita, Trans Nzoia laki tano na Vihiga laki nne.
Alisema hatua hiyo itawezesha eneo la Magharibi kuwa na takriban wapigakura milioni nne ambao watakuwa nguzo muhimu katika kumuunga mkono Rais Ruto katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.