Lugha, Fasihi na Elimu

Chama cha Uanahabari chawasha taa ya vipaji Kairi Boys

Na RICHARD MAOSI July 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHAMA cha Uanahabari katika Shule ya Upili ya Kairi Boys, Gatundu Kaskazini, Kaunti ya Kiambu, kinaendelea kuwa chombo muhimu cha kuwakuza wanafunzi kitaaluma na kitalanta huku kikiwafungulia milango katika fani zinazohusiana na lugha na mawasiliano.

Pamoja na kukuza vipaji vya wanafunzi katika sanaa hizo anuwai, chama hicho pia kinawapa msukumo wa kujitosa katika ualimu, tafsiri, upigaji picha na uhariri wa vitabu, video na filamu.

Isitoshe, kinalenga kuimarisha umilisi wa Kiswahili na Kiingereza ili kuwajenga wanafunzi wenye uwezo wa kujieleza kwa ufasaha kimazungumzo na kimaandishi.

Baadhi ya walimu wa Shule ya Upili ya Kairi Boys iliyoko Gatundu Kakazini, Kaunti ya Kiambu, walipojumuika kwa picha ya pamoja.

Wanachama hukutana baada ya vipindi vya masomo mchana kutwa ili kujadili mikakati ya kuendeleza chama na kukipa nguvu zaidi.

Aidha, chama kinatarajia kuanzisha kitengo cha uigizaji na kuzindua jarida rasmi la shule mwaka ujao, hatua itakayowapa wanafunzi jukwaa maridhawa la kuonyesha ubunifu wao katika uandishi na sanaa nyinginezo.

Mafanikio ya chama tayari yanaonekana.

Wanafunzi wanaoshiriki shughuli zake kikamilifu wamekuwa wakifaulu vyema katika mitihani ya Kiswahili na Kiingereza huku wakionyesha kujiamini zaidi katika mawasiliano na shughuli tofauti za shule.

Mlezi wa chama, Bi Doreen Kathurima, anaungama kuwa chama hicho kimechangia pakubwa maendeleo ya wanafunzi na kimekuwa chanzo cha mabadiliko muhimu shuleni.

“Mbali na kupiga jeki shughuli za Idara ya Lugha, chama hiki kinakuza maadili na kuboresha matokeo ya KCSE. Pia tumeshuhudia maendeleo makubwa katika ulumbi, utunzi wa mashairi na utangazaji wa habari miongoni mwa wanachama,” anaeleza.

Wanafunzi wa Shule ya Upili ya Kairi Boys wakifuatilia kwa makini matukio na mawasilisho mbalimbali wakati wa hafla ya kielimu waliyoiandaa. PICHA ZOTE | RICHARD MAOSI

Mwalimu Mkuu, Bw Anthony Mwaria, anakiri kuwa chama hicho kinawaandaa wanafunzi kwa ajili ya maisha ya baadaye.

“Chama hiki ni jukwaa linaloamsha hamu ya wanafunzi kujitosa katika ulingo wa uanahabari na taaluma nyingine zinazofungamana na lugha. Vilevile kinawalea na kuwakuza ipasavyo ili wawe watafiti na waandishi wabunifu wenye uwezo wa kushindana kimataifa,” anasema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Ushauri Nasaha, Bi Norah Biyaki, anasisitiza kuwa nidhamu na kujituma kwa wanafunzi ni msingi wa mafanikio ya chama.

“Tunawahimiza wanafunzi kuwa na ari ya kujifunza, nidhamu ya hali ya juu na moyo wa kujituma ili waweze kufaidika kikamilifu na fursa tofauti zinazotolewa na chama hiki,” akasema Bi Biyaki katika kauli inayotiliwa mkazo na Naibu Mwalimu Mkuu, Bw Michael Ngari.

Kupitia shughuli zake, Chama cha Uanahabari shuleni Kairi Boys kinaendelea kuwajenga wanafunzi kuwa wataalamu, viongozi na wasanii wa kesho.