Akili Mali

Aliishi bila ajira ila akapata wazo la kipato kupitia ukuzaji wa mboga kwenye matairi

Na KALUME KAZUNGU July 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

ZAHARA Mohamed, 45, ni mkazi wa kijiji cha Kauthara, tarafa ya Hindi, Kaunti ya Lamu.

Miaka kadhaa iliyopita, Bi Mohamed alikuwa akiishi bila kazi yoyote isipokuwa kutekeleza majukumu ya nyumbani tu kama mke, ikiwemo ulezi, kupika na kutunza nyumba.

Ila kwa sasa yeye ni mkulima na mfanyabiashara hodari wa mboga aliyejikimu binafsi.

Miongoni wa mimea anayopanda ni mchicha, spinachi, sukumawiki, hoho na mnavu.

Alipokea maarifa ya kupanda na kukuza mboga kutumia matairi kupitia elimu ya mitandaoni, hasa TikTok na YouTube.

Shughuli za kilimo chake cha mboga huzitekeleza bila matumizi ya dawa au kemikali.

Upekee wa mboga zake ni kwamba badala ya kunyunyiza kemikali, yeye huthamini sana matumizi ya michanganyiko asilia, ikiwemo majani ya mwembe na mwarobaini katika kupigana na wadudu waharibifu shambani.

Mbolea yake anayotumia pia ni ile ya mchanganyiko wa vitu kama vile mboji (compost) iliyooza na kutayarika vizuri.

Akiwa pia ni mfugaji kuku, mbuzi na kondoo, yeye hutumia sana kinyesi cha wanyama hao kama mbolea yake murua ya kikaboni, hivyo kuinawirisha mimea na bustani yake.

Mama huyo wa watoto watano alianza kilimo cha mboga kupitia matairi makuukuu mnamo 2024, akianza harakati zake akitumia gharama ya kwanza kabisa ambayo ilikuwa ni Sh6,000.

Miaka miwili baadaye, Bi Mohamed anakiri kuwa kilimo chake cha mboga ni biashara ya maana kwani humpatia kati ya Sh15,000 na Sh20,000 kwa mwezi.

Yeye husambaza mboga zake kila wiki kwa wafanyabiashara wa ndani ya soko la manispaa ya Hindi.

Hoteli nyingi na mikahawa ya mjini Hindi pia huodesha mboga zake.

Isitoshe, Bi Mohamed huzungusha bidhaa zake kwa pikipiki kwenye vijiji na vitongojini ambapo anakiri kuvuna pakubwa.

“Mimi situmii kemikali ya aina yoyote kutekeleza kilimo changu cha mboga. Nimeelekeza fikra na nguvu zangu zote kuendeleza kilimo hai. Hujihisi mwenye furaha ninapozalisha mboga ambazo ninajua hazina madhara yoyote kwa wateja wangu nikifahamu fika kwamba nimezikuza kwa njia asili kupitia kilimo hai,” akasema Bi Mohamed.

Wiki nzuri yeye huuza mboga za kati ya Sh4,000 na Sh5,000 kwani mara nyingi mavuno ya mboga kwenye bustani yake hupanda au kushuka.

“Sijuti kamwe kuanzisha mbinu hii ya kukuza mboga kwenye magurudumu ya zamani. Haya matairi huonekana na wengi kuwa ni takataka tu ila kwangu yamefaulisha kilimo na kunipa ajira,” akasema Bi Mohamed.

Ili kuhakikisha kuna usambazaji wa kutosha kwa maji kwenye mboga zake bustanini, Bi Mohamed amechimba kisima ambacho amekiunganisha kupitia mashini ya kupiga maji na mabomba.

Mboga anazouza sokoni na mitaani zimemwezesha kupata mtaji unaomsaidia kuchangia kukimu majukumu ya nyumbani, ikiwemo ununuzi wa chakula, kulipia watoto karo na mengineyo.

“Nashukuru. Kupitia kilimo cha mboga cha matairini, nimegeuzwa kutoka hali ya zamani ambapo nilikuwa mke wa nyumba tu. Nilimtegemea mume wangu kukidhi mahitaji yote ya nyumbani na yangu binafsi. Ila leo najisimamia mwenyewe kifedha na hata kumsaidia bwanangu kutekeleza baadhi ya majukumu ya kifamilia,” akasema Bi Mohamed.

Aliwashauri wakazi wa Lamu waliojikita katika mtazamo kwamba eneo hilo ni ngome ya uvuvi kama kitega uchumi cha pekee kuondoa fikra au dhana hiyo.

“Kupitia juhudi zangu nimebaini kuwa ukulima, hasa ule wa mboga na ufugaji hufanya vyema eneo hili letu. Badala ya kutegemea uvuvi, wajaribu kilimo na katu hawatajuta ilmuradi wawe wavumilivu,” akasema Bi Mohamed.

Afisa wa kilimo nyanjani wa serikali ya kaunti ya Lamu, Bw Lenox Katana anaeleza kuwa kupanda mboga kwenye matairi ya zamani ni njia nzuri, rahisi, na ya gharama nafuu ya kuanzisha bustani ya nyumbani, hasa kwenye maeneo madogo kama vile kwenye viwanja vya miji au mitaa ya miji kama vile Lamu, Malindi, Mombasa, Nairobi na kwingineko.

Bw Katana anataja manufaa ya kukuza mboga kwenye matairi makuukuu kuwa njia inayosaidia kuhifadhi unyevu na inayozuia mmomonyoko wa udongo.

Faida nyingine za matairi ni kuweka joto linalochochea ukuaji wa mimea.

Bw Katana anafafanua kuwa rangi nyeusi ya mpira wa matairi hufyonza joto la jua na kuufanya udongo kuwa wa uvuguvugu, jambo ambalo ni zuri kwa ukuaji wa mimea wakati wa baridi au nyakati za usiku.

Pia anaitaja mbinu hii ya kilimo kwamba inatoa uhuru wa mkulima kupanga bustani yake kwa mtindo wowote anaoutaka, hata ikiwa ni kwenye maeneo ya sakafu ngumu kama lami au zege.

Ila anashauri mkulima kwamba ni vyema kuhakikisha tairi limetobolewa mashimo chini ili kuruhusu maji ya ziada kupita na kuepusha kuoza kwa mizizi ya mimea.

“Kilimo cha mboga kutumia matairi makuukuu chaweza kutekelezwa hata kwenye vibaraza au pembezoni mwa nyumba yako katikati ya mji ambako mara nyingi ardhi kubwakubwa za kutekelezea kilimo zinakosekana,” akasema Bw Katana.

Katika kutekeleza uzalishaji mboga kwenye matairi ya zamani, Bw Katana anashauri kuhakikisha wakulima wanaweka udongo uliochanganywa vizuri na mbolea ndani ya matairi hayo.

Kinachofuata ni mja kuumwagilia udongo husika maji kabla ya kupanda mbegu au miche ya mboga kama vile spinachi, sukumawiki, vitunguu, nyanya nakadhalika.

Bw Katana anashauri kuwa kwa mimea yenye mizizi mirefu kama viazi vikuu, itakuwa ni vyema mkulima kuweka tairi mbili juu kwa juu kwenye bustani yake.