Ol Kalou: DCP ya Gachagua yabwaga UDA ya Ruto
Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imemtangaza Sammy Douglas Kamau Waweru Ngotho kuwa mshindi wa uchaguzi mdogo wa ubunge wa Ol Kalou baada ya kumshinda mpinzani wake mkuu kwa tofauti kubwa ya kura.
Bw Ngotho alipata kura 35,440 huku mpinzani wake mkuu, Muchina Nyaga wa chama cha United Democratic Alliance (UDA), akipata kura 5,460.
Afisa Msimamizi wa Uchaguzi, Anthony Njiraini, alitangaza matokeo hayo saa kumi na mbili Ijumaa alfajiri baada ya zoezi la kujumlisha kura lililodumu usiku kucha katika Shule ya Sekondari ya Ol Kalou, mjini Ol Kalou. Ni mgombea huyo wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP) na maajenti wake pekee waliohudhuria zoezi hilo.
Akihutubu kwa mara ya kwanza baada ya kutangazwa mshindi, mbunge huyo mteule alilaani ghasia zilizodaiwa kusababishwa na wahuni wanaoshukiwa kuwa maafisa wa polisi siku ya Alhamisi, hali iliyovuruga upigaji kura katika vituo vingi vya kupigia kura ndani ya mji wa Ol Kalou.
“Inasikitisha kwamba tumepoteza maisha kutokana na vurugu hizi za uchaguzi. Mmoja wa waliojeruhiwa, ambaye nilimfahamu vyema na alikuwa mfuasi wangu mkubwa, alifariki kutokana na majeraha yake. Wahuni hao pia waliwashambulia wanahabari wasio na hatia ambao silaha zao pekee zilikuwa kamera, simu na vijitabu. Inauma kwa sababu uhuni huu ulipangwa na kufadhiliwa na baadhi ya wabunge kutoka eneo la Mlima Kenya kwa usaidizi wa maafisa wakuu wa polisi,” alisema Bw Ngotho.
Alisema ushindi wake mkubwa ni ujumbe wazi kwa serikali kwamba imepoteza uungwaji mkono wa wananchi.
“Kilichotokea hapa kinaonyesha yatakayojiri mwaka ujao. Ninaishukuru IEBC kwa kazi nzuri. Ikiwa uchaguzi wa mwaka ujao utaendeshwa kwa namna hii, sina shaka kuwa Muungano wa Upinzani utashinda. Mmeonyesha sisi na Wakenya wote kuwa IEBC ni tume huru kweli,” alisema.
Pia, aliwapongeza maafisa wa polisi waliovalia sare rasmi, akisema walitekeleza wajibu wao kwa weledi.
Kamishna wa IEBC Hassan Noor aliwahakikishia Wakenya kuwa tume hiyo itaendesha uchaguzi ulio bora zaidi mwaka ujao.
“Zoezi hili limefanikiwa na tumepata mafunzo muhimu yatakayotusaidia kuboresha uchaguzi ujao. Ninawasihi wanasiasa waelekeze nguvu zao kwa wapigakura, si kwetu. Tuna IEBC moja pekee, na tunafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha uchaguzi wa mwaka ujao utakuwa huru na wa kuaminika,” alisema kamishna huyo.
Seneta wa Nyandarua John Methu, aliyeratibu kampeni za mgombeaji wa DCP, pia alilaani vurugu hizo akisisitiza kuwa waliowashambulia wananchi walikuwa maafisa wa polisi.
“Ninamtaka Inspekta Jenerali wa Polisi awakamate na kuwafikisha mahakamani wahuni hawa. Tuna sura zao, taarifa zao na video zinazowaonyesha wakitekeleza vitendo hivyo. Ukiwakamata utakuwa umeitumikia Kenya kwa uadilifu. Usipofanya hivyo, utakuwa umeacha nchi hii kuelekea pabaya,” alisema Seneta Methu.
Bi Jedidah Muchoki, mwanasiasa kutoka Ndia aliyefuatilia uchaguzi huo kwa niaba ya mgombeaji wa DCP, alisema polisi wanapaswa kuwadhibiti wahuni hao kabla hali haijawa mbaya zaidi.
“Tunawashukuru wapigakura wa Ol Kalou kwa jinsi walivyoendesha uchaguzi kwa amani. Uchaguzi ulikuwa wa utulivu hadi wahuni walipoingilia kati. Ushindi mkubwa wa DCP unaonyesha wazi kuwa Wakenya wamechoshwa na serikali hii. Serikali hii haiwezi kujirekebisha na inapaswa kuhudumu kwa muhula mmoja tu,” alisema Bi Muchoki, ambaye pia analenga kuwania kiti cha eneo bunge la Ndia.