Habari

Ushindi wa Gachagua Ol Kalou wazua mjadala kuhusu mgawanyiko Mlimani

Na Na DAVID MUCHUI July 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRI wa Utumishi wa Umma, Geoffrey Ruku, amesema matokeo ya uchaguzi mdogo wa Ol Kalou hayana athari kwa siasa za Mlima Kenya Mashariki, akisisitiza kuwa eneo hilo limeamua kuendelea kumuunga mkono Rais William Ruto.

Kauli hiyo ilitolewa Alhamisi ilipobainika kuwa mgombea wa chama cha DCP alikuwa akielekea kupata ushindi mkubwa dhidi ya mgombea wa UDA.

“Sisi wa Mlima Kenya Mashariki hatujali kinachotokea Mlima Kenya Magharibi,” alisema Bw Ruku.

Kwa miezi sita iliyopita, Bw Ruku amekuwa akihimiza kaunti za Kirinyaga, Embu, Tharaka Nithi na Meru kujitenga kisiasa na eneo la Mlima Kenya Magharibi.

Hatua hiyo inaonekana kuwa mkakati wa kuimarisha ushawishi wa Rais Ruto katika eneo hilo huku ikizuia juhudi za aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kuunganisha Mlima Kenya chini ya DCP.

Bw Ruku anaamini kuwa eneo la Mlima Kenya Mashariki linaweza kutoa zaidi ya kura milioni mbili na hivyo kuwa na nguvu kisiasa.

Hata hivyo, mchambuzi wa siasa Profesa Gitile Naituli amesema siasa za Kenya haziamuliwi na jiografia pekee.

“Wazo kwamba Mlima Kenya Mashariki una umuhimu tu unapomuunga mkono Mkikuyu kutoka Magharibi ni rahisi mno. Historia ya Kenya inaonyesha kuwa ushindani wa kisiasa, maafikiano ya viongozi na miungano ndiyo huamua matokeo,” alisema.

Aliongeza kuwa uchaguzi mdogo wa Ol Kalou ni kipimo cha hali ya kisiasa nchini na unaweza kuashiria mwelekeo wa uchaguzi mkuu wa 2027.

Baada ya matokeo hayo, Naibu Rais Kithure Kindiki aliandika kwenye Facebook kuwa ni wakati wa “kurudi kujipanga upya .”

Wiki iliyopita Prof Kindiki aliwahimiza wakazi wa Meru kuendelea kumuunga mkono Rais Ruto, akisema kura kwa rais ni kura kwake pia.

“Hapa Meru hatuna chaguo lingine isipokuwa kumpigia kura Rais Ruto mwaka 2027. Kumpigia kura William Ruto ni kunipigia kura mimi,” alisema.

Mnamo Jumatatu, Bw Ruku alikutana na zaidi ya vijana 300 kutoka Embu, Meru, Isiolo na Tharaka Nithi kuhimiza kampeni ya kujitegemea kisiasa kwa Mlima Kenya Mashariki.

Alisema watahakikisha upinzani haupati nafasi katika eneo hilo.

“Tutaweka mpaka kati ya Mlima Kenya Mashariki na Magharibi. Hatutampa Gachagua nafasi ya kujitanua huku mashariki,” alisema.

Aidha, madiwani 61 wa Bunge la Kaunti ya Meru walitangaza kuendelea kumuunga mkono Rais Ruto na Prof Kindiki, wakisema kaunti hiyo imenufaika na miradi ya maendeleo.

Lakini ushindi wa DCP Ol Kalou unaonekana kumpa Bw Gachagua nguvu mpya.

Aliyekuwa Mbunge wa Nyeri Ngunjiri Wambugu alisema ushindi huo unaweza kumfanya Bw Gachagua kuwa mwanasiasa mwenye ushawishi mkubwa katika Mlima Kenya.

“Huo ushindi unaweza kumfanya Gachagua kuwa na nguvu kubwa kisiasa. Wale ambao hatuwezi kufanya kazi naye lazima tukae chini na kupanga upya mikakati yetu,” alisema.

Kwa upande wake, Bw Gachagua ameendelea kusisitiza kuwa hataruhusu juhudi zozote za kugawa kisiasa eneo la Mlima Kenya.