Gachagua kuwinda ngome ya Kindiki baada ya Ol Kalou kumweka roho juu
SIKU chache baada ya kupata ushindi katika uchaguzi mdogo wa eneobunge la Ol Kalou, aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua sasa ameelekeza juhudi zake Mlima Kenya Mashariki katika kile wachambuzi wa siasa wanasema ni mkakati wa kupanua ushawishi wake tayari kwa uchaguzi mkuu wa 2027.
Baada ya mgombea wa chama chake cha DCP, Sammy Waweru, kushinda kwa kishindo uchaguzi mdogo wa Ol Kalou, Bw Gachagua anaamini tayari amejijengea msingi imara katika Mlima Kenya Magharibi.
Sasa analenga kuzima ushawishi wa Prof Kindiki katika kaunti za Meru, Embu na Tharaka Nithi, ambazo zimeendelea kuwa ngome muhimu ya Kenya Kwanza.
Katika juhudi hizo, Bw Gachagua ametangaza ziara ya siku sita katika kaunti za Meru na Embu, hatua inayotajwa kuwa kubwa zaidi ya kisiasa katika eneo linalohusishwa na Prof Kindiki.
Hatua hiyo imejiri siku chache baada ya Bw Gachagua kumtetea hadharani Prof Kindiki dhidi ya viongozi wa Kenya Kwanza wanaotaka kugawa Mlima Kenya katika sehemu mbili za Mashariki na Magharibi.
Aliwataka wafuasi wake wasimshambulie binafsi Naibu Rais, akisisitiza kuwa Mlima Kenya unapaswa kubaki na umoja wa kisiasa.
Hata hivyo, wachambuzi wanasema msimamo huo si wa maridhiano bali ni mkakati wa kutuliza hali ya kisiasa kabla ya kuanza kampeni katika Mlima Kenya Mashariki.
Mchambuzi wa siasa John Anditi alisema Bw Gachagua anataka kuwavutia wapigakura wa Mashariki kabla ya Prof Kindiki kuimarisha zaidi ushawishi wake.
“Anajaribu kujionyesha kama mtetezi wa umoja wa Mlima Kenya huku akizuia eneo hilo kugeuka ngome ya UDA pekee,” alisema.
Matokeo ya chaguzi ndogo yameonyesha mgawanyiko wa kisiasa katika eneo hilo.
Huku DCP ikishinda Ol Kalou, UDA ilitwaa kiti cha ubunge cha Mbeere Kaskazini na viti vya wadi za Evurore na Muminji mwaka jana, hali iliyofasiriwa kama ushahidi kuwa Prof Kindiki bado ana ushawishi mkubwa Mashariki.
Kutokana na hali hiyo, Mlima Kenya sasa umegawanyika katika mirengo miwili ya kisiasa. Mlima Kenya Magharibi, unaojumuisha Nyeri, Nyandarua, Murang’a, Kiambu na sehemu za Nakuru, unaonekana kuegemea upande wa Bw Gachagua.
Mashariki, inaohusisha Meru, Embu na Tharaka Nithi ndiko Prof Kindiki anaongoza uimarishaji wa ufuasi wa Kenya Kwanza.
Kwa Rais Ruto, hali hiyo inaleta changamoto na fursa kwa wakati mmoja.
Ingawa Prof Kindiki amezuia kuporomoka kwa uungwaji wa UDA katika Mlima Kenya Mashariki, ushawishi wa Bw Gachagua Magharibi unatishia muungano uliomuingiza Dkt Ruto mamlakani mwaka wa 2022.
Wakili Nelson Osiemo alisema hatua ya Bw Gachagua inalenga kuunganisha Mlima Kenya na kujijenga kama msemaji mkuu wa eneo hilo.
Alisema ndiyo sababu amekuwa na mikutano na mgombea urais wa chama cha Safina Jimi Wanjigi na kuzungumza vyema kuhusu Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta pamoja na Prof Kindiki.
Wakati huo huo, Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku amependekeza Mlima Kenya Mashariki ujitafutie mwelekeo wake wa kisiasa iwapo viongozi wa Magharibi hawatamuunga Prof Kindiki.
Kauli hiyo imepingwa na Waziri wa Ardhi Alice Wahome, aliyesema Mlima Kenya haupaswi kugawanywa kwa misingi ya kisiasa.
Mchambuzi wa siasa Dismas Mokua anaamini Bw Gachagua anajijenga kama kiongozi mkuu wa kisiasa wa Mlima Kenya.
“Anataka kuonekana kuwa ndiye mwenye uwezo wa kuwalinda viongozi wa Mlima Kenya na kuwaunganisha,” alisema.