Familia ya Sharon Otieno yafurahia uamuzi na kusema ni ukurasa mpya
FAMILIA ya Sharon Otieno imesema imepata afueni baada ya Mahakama Kuu kumpata na hatia aliyekuwa Gavana wa Migori Okoth Obado pamoja na wasaidizi wake wawili kwa mauaji ya binti yao, ikisema hukumu hiyo ni mwanzo wa ukurasa mpya baada ya kusubiri haki kwa karibu miaka minane.
Akizungumza kwa simu na Taifa Dijitali Ijumaa, baba yake Sharon, Douglas Otieno, alisema ingawa haki imepatikana, hukumu hiyo imefufua maumivu ya kumpoteza binti yao.
“Hata kama haki imetendeka na tunahisi afueni kidogo, bado hukumu hii imeturudisha kwenye maumivu ya zamani. Ni kana kwamba jeraha limetoneshwa. Tulikuwa mahakamani jana na hali ilikuwa ya kutuumiza sana kisaikolojia,” alisema.
Aliongeza kuwa familia sasa inaona mwanzo mpya baada ya kusubiri haki kwa miaka minane.
Douglas Otieno na mkewe Melida Auma walizungumza kabla ya kurejea nyumbani kwao Homa Bay, wakisema sasa wanafahamu waliohusika na mauaji ya binti yao