Sifuna apokelewa kishujaa Magharibi, Wantam ikitanda hewani
ENEO la Magharibi limegeuka uwanja mkuu wa mapambano ya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027, huku Rais William Ruto na viongozi wa upinzani wakilenga zaidi ya milioni 3.3.
Magharibi kwa sasa ina jumla ya wapigakura waliosajiliwa milioni 2.92 katika kaunti tano, na inachukuliwa kuwa ngome muhimu inayoweza kuamua mshindi wa urais. Kufikia 2027, eneo hilo lenye kaunti za Bungoma, Kakamega, Trans Nzoia, Vihiga na Busia litakuwa na zaidi ya kura milioni 3.3.
Katika uchaguzi wa 2022, Rais Ruto alipata ushindi mkubwa katika Kaunti ya Bungoma kwa kura 255,906, dhidi ya kura 145,280 za aliyekuwa mpinzani wake Raila Odinga. Matokeo hayo yalimsaidia kuingia Ikulu kwa tofauti ndogo ya kura.
Sasa, ikiwa zimesalia chini ya miezi 12 kabla ya uchaguzi mkuu, vita vya kuhifadhi au kurejesha kura hizo vimeanza rasmi.
umapili, Kiongozi wa kundi la Linda Mwananchi na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna alikamilisha ziara ya siku mbili katika kaunti za Bungoma na Trans Nzoia huku Rais Ruto akiwa katika Kaunti ya Busia akizindua na kukagua miradi ya maendeleo.
Pande zote mbili zilijitokeza zikisisitiza kuwa zinaungwa mkono na wakazi wa Magharibi.
Katika mikutano yake, Bw Sifuna aliendelea kujisawiri kama mgombeaji anayetarajia kupeperusha bendera ya upinzani katika uchaguzi wa urais wa 2027, huku akiwataka wakazi wa Magharibi wasimwache njiani.
“Watu wengi wanasema mnanipigia debe tu. Mmenihimiza niende hadi kwenye debe? Msije mkaniacha njiani. Simameni nami ili nikabiliane na Rais William Ruto uso kwa macho,” akasema
Alisema kundi la Linda Mwananchi limezunguka maeneo mengi nchini na kupokea ahadi za kuungwa mkono.
“Nimeunda kikosi imara kutoka Pwani, Mlima Kenya, Nyanza, Magharibi na maeneo mengine. Kwa mapenzi ya Mungu, ndani ya miezi 12 tutakuwa tumekamilisha safari yetu kuelekea Ikulu,” akaongeza.
Bw Sifuna alisema safari yake ya kisiasa ilianzia Magharibi alipojaribu kuwania ubunge wa Kanduyi kabla ya marehemu Raila Odinga kumlea kisiasa na kumwezesha kuwa Seneta wa Nairobi, Katibu Mkuu wa ODM na Kiranja wa Wachache katika Seneti.
Aidha, alidai kuwa viongozi wanaomuunga mkono Rais Ruto wanampotosha kwa kumwambia anaungwa mkono Bungoma.
“Kuna watu wanamdanganya Rais kuwa ana kura Bungoma. Ukweli ni kwamba hana kura hapa. Safari ya mabadiliko tayari imeanza,” akasema.
Ziara hiyo ilihudhuriwa na Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi na Waziri wa zamani Musikari Kombo ambaye alihudumu katika utawala wa marehemu Rais Mwai Kibaki.
Tangu asubuhi, mamia ya wafuasi walifurika mjini Bungoma wakiwa na mabango yenye picha ya Bw Sifuna huku wakiimba nyimbo za jadi za Bukusu na nyimbo zilizokuwa zikitumika katika kampeni za marehemu Raila Odinga.
Msafara huo ulianza kwa ibada katika Kanisa Kuu la St Immaculate mjini Kitale kabla ya kupitia Kiminini, Sikhendu, Kamukuywa, Kimilili, Chwele na Kanduyi.
Katika ishara ya kumuunga mkono, wakazi walichangia kati ya Sh50 na Sh1,000 kufanikisha kampeni zake za urais.
“Afadhali nidaiwe Sh10 na kila mwananchi wa Bungoma kuliko kudaiwa na tajiri mmoja ambaye baadaye atanitaka nimlipe kwa zabuni nikichaguliwa,” akasema Bw Sifuna.
Aliahidi kuwa serikali ya upinzani itafuta Ushuru wa Nyumba, ushuru wa mafuta na kodi nyingine alizosema zimekuwa mzigo kwa wananchi.
Kwa upande wake, Gavana Natembeya alisema Magharibi imekuwa ikikosa nafasi za kisiasa kutokana na migawanyiko ya viongozi wake, akitoa wito wa kuungwa mkono kwa mgombeaji mmoja wa urais.
“Historia yetu imejaa migawanyiko. Watu walidhani mimi na Sifuna tungepambana, lakini tuliketi na kukubaliana. Wenzangu wa upinzani wawe jasiri na waseme wazi, ‘Sifuna tosha’,” akasema Bw Natembeya.
Aliwataka pia viongozi wa Nyanza kuunga mkono mgombeaji kutoka jamii ya Mulembe kama walivyofanya kwa Raila Odinga kwa miaka mingi.
Viongozi hao pia waliwashambulia Gavana wa Bungoma Kenneth Lusaka na Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa, kwa kumpotosha Rais Ruto kuwa
Bw Natembeya alisema serikali ya upinzani itafuta Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), Ushuru wa Nyumba, Mtaala wa Umilisi na Utendaji (CBC) na kodi nyingine alizodai zinawaumiza raia.
Gavana Orengo alisema safari ya upinzani kuelekea Ikulu haiwezi kuzuiwa isipokuwa kupitia wizi wa kura, huku Seneta Osotsi akitaka kizazi kipya cha viongozi kupewa nafasi Magharibi.
Naye Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino alisema Linda Mwananchi tayari imefanya ziara katika kaunti 16 na inalenga kufika kaunti zote 47 kabla ya 2027.
Alisema baada ya Magharibi, kundi hilo litaelekea Nyanza, Kisii, Mlima Kenya na Ukambani kukutana na viongozi wa upinzani akiwemo Fred Matiang’i, Rigathi Gachagua na Kalonzo Musyoka ili kuunda muungano mmoja utakaompinga Rais Ruto mwakani.