Besigye mahututi ICU, mkewe Winnie Byanyima athibitisha
KAMPALA, Uganda:
MWANASIASA mashuhuri wa upinzani Uganda, Kizza Besigye, anaendelea kulazwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi (ICU) katika Hospitali ya Kitaifa ya Rufaa ya Mulago baada ya kuzimia akiwa mahakamani jijini Kampala mnamo Jumatano.
Mkewe, Winnie Byanyima, alithibitisha taarifa hiyo kupitia ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa X mapema Alhamisi, akisema mwanasiasa huyo, 70, alikuwa amepoteza fahamu na hali yake ya afya ilikuwa mbaya.
“Amepoteza fahamu, hawezi kuzungumza na hata maumivu yakimlemea hagutuki,” akasema Byanyima, ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kupambana na Ukimwi (UNAIDS).
Besigye alizimia alipofika mahakamani jijini Kampala, ambako anakabiliwa na mashtaka ya uhaini. Baadaye aliondolewa mahakamani kwa gari la wagonjwa na kukimbizwa hospitalini.
Msemaji wa serikali ya Uganda, Alan Kasujja, hakujibu jumbe au simu ili kutoa maoni kuhusu tukio hilo.
Kiongozi huyo mkongwe wa upinzani amekuwa rumande tangu Novemba 2024 baada yake na msaidizi wake, Obeid Lutale, kukamatwa Kenya kabla ya kurejeshwa Uganda, ambako baadaye walishtakiwa kwa kosa la uhaini.
Mawakili wake, wafuasi na wanaharakati wa haki za binadamu wamekuwa wakipinga mashtaka hayo wakisema yana msukumo wa kisiasa.
Wanasema kuendelea kuzuiliwa kwake ni mbinu ya serikali ya kuwazima wakosoaji wa utawala wa Rais Yoweri Museveni.
Rais Museveni, 81, alitangazwa mshindi wa uchaguzi mkuu wa Uganda uliofanyika Januari.
Matokeo hayo yalikataliwa na mpinzani wake mkuu Bobi Wine, ambaye tangu wakati huo ameishi uhamishoni Amerika.
Kuzuiliwa kwa Besigye kumezua wasiwasi mkubwa katika mataifa mbalimbali duniani.
Ingawaje, anafahamika kama mmoja wa viongozi wachache waliothubutu kumpinga Rais Museveni katika utawala wake wa miongo kadhaa Uganda.