Orengo amrai Jumwa aingie wantam baada ya kumtema Ruto
KIONGOZI wa vuguvugu la Linda Mwananchi, Bw James Orengo, amemkaribisha rasmi aliyekuwa Waziri wa Masuala ya Jinsia, Bi Aisha Jumwa, kujiunga na upinzani katika juhudi za kumuondoa Rais William Ruto mamlakani kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Bw Orengo alisema kujiunga kwa Bi Jumwa kutaimarisha ushawishi wa vuguvugu hilo katika eneo la Pwani kutokana na tajriba na ushawishi wake wa kisiasa.
Bw Orengo alisema anaheshimu uamuzi wa Bi Jumwa wa kuendelea na mashauriano kabla ya kutangaza msimamo wake wa kisiasa, lakini akasisitiza kuwa milango ya Linda Mwananchi iko wazi kwake.
Hata hivyo, aliongeza kuwa iwapo Bi Jumwa ataamua kujiunga na vuguvugu hilo, atapewa nafasi ya juu ya uongozi, huku akidai kuwa viongozi wengi wa Pwani wako tayari kuondoka UDA na kujiunga na upinzani kuelekea uchaguzi wa mwaka 2027.
Hatua hiyo inajiri siku moja baada ya Bi Jumwa kutangaza kujiondoa katika chama cha Rais William Ruto, akitaja kile alichodai kuwa ni vitendo visivyo vya kidemokrasia vinavyodhoofisha matakwa ya wananchi wa Kilifi.
Mbunge huyo wa zamani wa Malindi alisema alifikia uamuzi huo baada ya mashauriano na wakazi wa Kilifi, kutafakari na kufanya maombi.
Bi Jumwa, ambaye ni mmoja wa waanzilishi wa UDA, alisema kuondoka katika chama hicho halikuwa jambo rahisi kwa kuwa alitumia nguvu na kujitolea kukijenga chama hicho.
Hata hivyo, kwenye mkutano na Bw Orengo, Bi Jumwa alisema bado anaendelea na mashauriano na vyama mbalimbali vya kisiasa kabla ya kutangaza msimamo wake kuhusu chama atakachotumia kuwania ugavana wa kaunti ya Kilifi mwaka 2027.
“Leo nimetembelewa na Gavana James Orengo na tumekuwa na mazungumzo yenye manufaa. Nilipotoa taarifa ya kujiondoa UDA nilisema niko tayari kuzungumza na watu wenye mawazo yanayofanana na yangu kwa manufaa ya watu wa Kilifi, pwani na taifa kwa ujumla. Bado naendelea kushauriana na wananchi wa Kilifi na pwani kabla ya kufanya uamuzi wa mwisho, lakini ninaamini siku zijazo zitakuwa njema,” alisema Bi Jumwa.
Bw Orengo, ambaye pia ni Gavana wa Siaya, alisema mara tu alipopata taarifa za kujiondoa kwa Bi Jumwa kutoka UDA, aliamua kumtafuta haraka na kumshawishi kujiunga na Linda Mwananchi.
“Kama kiongozi wa Linda Mwananchi, sikuona sababu ya kupoteza muda. Bi Jumwa alikuwa mmoja wa washirika wa karibu wa kinara wa ODM Raila Odinga. Kila alipokuwa akifanya mikutano ya kisiasa, Bi Jumwa alikuwa mstari wa mbele. Baba alimpa jina la Mekatilili wa Menza kutokana na ujasiri wake. Ninaamini alipo Bw Odinga anafurahia kuona tukishirikiana tena,” alisema Bw Orengo.
Aliwataka wakazi wa Mombasa, Kilifi, Kwale, Lamu, Tana River na Taita Taveta kumuunga mkono Bi Jumwa, akimtaja kuwa mwanasiasa shupavu, mzungumzaji mahiri na mwenye uwezo wa kuongoza.
“Pwani sasa imepata kiongozi ambaye anaweza kutetea maslahi ya wananchi wake. Wapwani wengi wanaunga mkono ajenda ya mabadiliko, lakini baadhi ya viongozi wamekuwa na hofu ya kujitokeza hadharani. Uamuzi wa Bi Jumwa utawapa wengine ujasiri wa kujiunga nasi,” alisema.
Aliongeza kuwa Linda Mwananchi tayari imeanza kujipanga kwa uchaguzi wa 2027 na ina imani kuwa itashinda.
“Tutasimama kidete kumlinda mtoto wetu wa Pwani. Bi Jumwa ni kiongozi ambaye amepitia changamoto nyingi za kisiasa lakini ameendelea kusimama imara. Tunahitaji Pwani iungane na vuguvugu letu,” alisema.